Ni jambo lisilokuwa na ubishi kwamba wengi wetu tunatamani kubadili maisha yetu ili yawe bora zaidi. Katika harakati zetu za kuboresha maisha yetu tunafanya mambo mengi lakini wakati mwingine hatupati majibu tuliyotegemea. Hii inatokana na kutokujua baadhi ya vitu muhimu tunavyotakiwa kufanya.

Kuwa na malengo na mipango ni jambo muhimu ili kubadili maisha, kufanya jambo la kukusogeza kwenye malengo yako pia ni muhimu sana ili kutoka ulipo. Pamoja na vitu hivi kuna kitu kimoja cha muhimu sana kufanya ili kuweza kufanikiwa kwenye safari ya kuboresha maisha yako.

learn

Kabla ya kujua kitu hicho hebu tuangalie mifano michache. Kuna watu wengi wana taaluma nzuri tu kama uinjinia, udaktari, usanifu na wanafanya vizuri sana kwenye taaluma hizo ila maisha yao nje ya taaluma hizo yanakuwa magumu sana. Hata wanapojaribu kufanya kitu cha ziada kama biashara zinazohusisha taaluma zao wanashindwa kupata majibu mazuri, unajua kwa nini?

Bill Gates ambaye ni mtu tajiri sana duniani ana taaluma ya kutengeneza program za kompyuta. Pamoja na kwamba amefanikiwa sana kupitia program za kompyuta yeye sio kwamba anajua sana kompyuta kushinda watu wengine duniani.

Mmiliki wa Facebook bwana Mark Zuckerberg naye anautaalamu wa sayansi ya kompyuta, pamoja na kufanikiwa sana kwa kupitia kompyuta sio kwamba yeye ndiye anaijua sana kompyuta kushinda watu wengine.

Ili ufanikiwe kwenye chochote unachofanya unahitaji kujifunza vitu vipya na vitu vya ziada. Hivyo sehemu ya kwanza ya kuboresha maisha yako ni kujifunza vitu vya ziada.

Bila ya kujali taaluma yako kuna vitu ambavyo ni vya muhimu sana unatakiwa kujifunza ili uweze kufanikiwa.

1. Jifunze kuhusiana na uongozi. Hii itakusaidia kuweza kufanikiwa kwenye kazi unayofanya na kukuwezesha kujenga biashara na kuwa kubwa. Watu wanapenda kufuata viongozi, hivyo kwa kuwa na sifa za uongozi unaweza kuwa na wafuasi wengi watakaokufanya ufanikiwe.

2. Jifunze kuhusu hela na mzunguko wa hela(cashflow). Hii itakusaidia sana kuweza kusimamia hela zako binafsi na za biashara yako.

3. Jifunze kuhusu mauzo na masoko(sales and marketing). Hata kama hufanyi biashara kujua kuhusu masoko na mauzo itakusaidia sana kwenye chochote unachofanya. Kuna kitu fulani unakiuza kwenye maisha yako, inaweza kuwa muda, ushawishi au mawazo, ili uweze kufanikiwa ni vyema kujua mbinu za masoko na mauzo.

4. Mbinu za biashara kwa ujumla. Kama upo kwenye biashara au unafikiri kuna siku utakuja kuingia kwenye biashara basi ni vyema ukachukua muda na kuanza kujifunza/kujisomea kuhusu biashara.

5. Jifunze kuhusu kompyuta. Hii ni taaluma moja ambayo hutakiwi kuacha kuijua kama unataka kufanikiwa. Jifunze kwa kiwango kidogo kuhusiana na utengenezaji program za kompyuta, mitandao na utengenezaji wa picha. Pia jua program za msingi za kompyuta na matumizi yake kwa kazi au biashara unayofanya.

6. Jifunze kuhusu mitandao ya kijamii na mbinu nyingine za masoko ya kwenye mtandao. Kama unafanya kazi au biashara ambayo unaweza kupata wateja kupitia mtandao(karibu biashara zote inawezekana) basi ni vyema ujifunze kuhusu masoko ya kwenye mitandao na mitandao ya kijamii. Hii itakusaidia kupata wateja wengi kupitia mtandao.

7. Jifunze kuhusu maendeleo binafsi na ujihamasishe. Hakuna kitu muhimu kama maendeleo yako wewe binafsi na ili biashara yako ikue ni muhimu ukue wewe kwanza. Jifunze mbinu mbalimbali za kuwa mtu bora na ujihamasishe. Hii itakusaidia kuzivuka nyakati ngumu.

8. Jifunze kuhusu saikolojia ya watu. Ili kuweza kwenda na watu vizuri ni muhimu kuwa na uelewa japo kidogo kuhusiana na saikolojia ya binadamu.

Hivi ni baadhi ya vitu vya msingi ambavyo kila mtu anatakiwa kujifunza japo kwa kiwango kidogo. Watu wengi wanafikiri ukishakuwa na taaluma moja kama uinjinia au udaktari inatosha. Hii ndio sababu kubwa unakuta watu wengi wenye taaluma fulani wana uelewa mkubwa na wanafanya kazi kwa bidii sana ila maisha yao bado yanakuwa magumu

Ili uboreshe maisha yako ni muhimu ujifunze vitu vya ziada vitakavyokufanya uweze kuwa na uwanja mpana zaidi wa kufanya maamuzi.

Unawezaje kujifunza vyote hivi? Baadhi ya vitu hivyo unajifunza hapa AMKA MTANZANIA na kuna vitabu mbalimbali nimekuwa nikituma kwa watu walioko kwenye mtandao huu. Kama unashindwa kusoma vitabu vingi unaweza kuwa unajifunza vitu hivi kidogo kidogo kwenye KISIMA CHA MAARIFA. Kujua kuhusu kisima cha maarifa bonyeza maandishi haya.

Pia unaweza kuanza kwa kusoma kitabu KWA NINI MPAKA SASA WEWE SIO TAJIRI na kuanza kuona sababu zinazokuzuia kufikia utajiri. Kupata kitabu hiki bonyeza maandishi haya.

Unapata wapi muda wa kufanya yote haya? Unaweza kupata muda wa kutosha kujifunza vitu vyote hivi, bonyeza hapa kujua zaidi.

Kwa vyovyote unavyofanya hakikisha vitu hivyo muhimu unavijua na unaweza kuvichanganya na taaluma yako ili kuboresha maisha yako.