Mara nyingi watu wamekuwa wakiuliza ni biashara gani inalipa ambayo wanaweza kufanya na wakapata mafanikio. Jibu la uhakika ni kwamba kila biashara inalipa(soma; hii ndio biashara inayolipa sana)

  Hata baada ya kujua biashara itakayokulipa ni ile unayopendelea kufanya(kama umesoma hapo juu) bado kuna changamoto ya kuja na wazo zuri la biashara. Nina hakika umewahi kuwa na fedha kidogo na kutamani kuiweka kwenye biashara ila ukashindwa kujua ufanye biashara gani.

  Ili biashara yoyote iweze kusimama ni lazima iwe na nguzo tano muhimu. Nguzo ya kwanza ni kutengeneza thamani. Ili biashara ianze na kukua ni lazima iweze kutengeneza thamani ambayo watu watakuwa tayari kutoa fedha zao ili kuipata. Thamani hiyo inaweza kuwa ni bidhaa au huduma. Hapa nitazungumzia jinsi ya kuja na wazo la kutengeneza thamani ambayo watu watakukimbilia kukupa fedha. Kujifunza nguzo nyingine nne zilizobakia nenda kwenye KISIMA CHA MAARIFA. Kama bado hujajiunga na kisima bonyeza maandishi haya kupata maelezo ya kisima.

Jua tatizo linalosumbua watu na tafuta njia ya kulitatua.

Biashara zote kubwa duniani zimejengwa kwenye msingi mmoja tu, kutatua matatizo yanayosumbua watu.

  Watu walikuwa na tatizo la kushindwa kuwasiliana na wenzao wa mbali ndipo biashara za mawasiliano na usafiri zikaanzishwa na kukua kwa kasi.

  Kama umewahi kuumwa au kuwa na mgonjwa utakuwa unaelewa vizuri kwamba hata kama mtu ana shida ya fedha kiasi gani linapokuja tatizo la afya atatafuta kila njia ili aweze kulitatua.

  Hivyo hata watu wawe na shida ya fedha kiasi gani wako tayari kulipia kitu ambacho kitawaondolea tatizo linalowasumbua. Hapa ndipo penye wazo kubwa la biashara.

kitabu kava tangazo

 

Tengeneza wazo lako la biashara kutokana na matatizo ya watu.

Kwa kuwa inabidi ufanye biashara ambayo unaipenda na kwa kuwa unahitaji ubunifu ili biashara yako iweze kukua fikiria wazo lako la biashara kutokana na matatizo ya watu.

  Angalia vitu ambavyo unapenda kufanya kutokana na vipaji vyako. Pia angalia ujuzi ambao unao na elimu uliyopata kwenye kada fulani. Kisha angalia ni matatizo gani watu wanayapata na unaweza kuyatatua. Jinsi ambavyo tatizo ni kubwa ndivyo thamani ya biashara inavyozidi kuwa kubwa.

  Kwa njia yoyote ile kuna bidhaa au huduma unaweza kuitoa na ikatatua matatizo ya watu.

  Makampuni na biashara zote kubwa zimekuwa zikihangaika kutafuta jinsi ya kutatua matatizo ya watu na kujenga biashara kubwa.

Wakati mwingine watu hawajui tatizo mpaka waone suluhisho.

Sio kila mara watu watakuwa wanajua matatizo yao, kuna wakati mwingine watu wanakuwa hawajui kama wana tatizo mpaka waone kuna njia rahisi ya kufanya mambo, hii inaitwa ujinga wa soko.

  Hivyo kama wewe unaona kuna njia bora ya kuboresha maisha ya watu tengeneza biashara yako na washawishi watu. Kama wakitumia na kuona ina faida kwao watakuwa wateja wako na watawaambia wengine pia. Hivi ndivyo mitandao ya kijamii kama facebook na twitter ilivyoteka soko. Mwanzo hakuna mtu alidhani kuna uhitaji mkubwa wa mitandao ya aina hii, kabla ya kuanza kwa facebook sikuwahi kuona watu wakilalamika kwamba wanahitaji facebook. Ila baada ya mitandao hii kuwepo na watu wakaanza kuitumia imewawia vigumu kuacha kuitumia. Kila siku tunashuhudia ni jinsi idadi ya watumiaji wa mitandao hii inavyoongezeka.

 

  Usilalamike tena kuhusu ni wapi unaweza kupata wazo bora la biashara. Anza kwa kuangalia ni tatizo gani ambalo watu wanalo na unaweza kulitatua. Au ni njia gani unaweza kurahisisha maisha ya watu wengine. Ukiweza kufikiri hivi wenye uhitaji wataanza kukukimbilia kukupa fedha ili matatizo yao yatatuliwe.

  Kwa mengi zaidi kuhusu biashara, teknolojia na maisha jiunge na kisima cha maarifa. Bonyeza maandishi haya kupata maelezo kuhusu kisima cha maarifa.