Pamoja na kuwepo njia mbalimbali za kuzingatia katika kuanzisha na kuendesha biashara bado biashara nyingi zimekuwa hazifanyi vizuri. Tambua kuwa kuanzisha na kuendesha biashara si jambo rahisi ni lazima uwe na nidhamu ,bidii na uwe tayari kujifunza hili uweze kupata mafanikio katika biashara unayofanya .Watu wengi hugundua ugumu wa kuendesha biashara baada ya kuanza na si kabla.

biashara7

Kuna baadhi ya watu ambao wanachukulia suala la Ujasiriamali kama jambo jepesi kwa sababu tu wana uwezo wa kupata mitaji. Wanafikiri wanaweza kufanya chochote na kupata mafanikio katika biashara, kumbe kuna mambo mengi ya kuangalia. Zifuatazo ni sababu 5 muhimu kwa nini biashara nyingi huwa hazifanyi vizuri

1. Kukosekana kwa mpango bora wa biashara

Je umejipanga vipi kibiashara? Wajasiriamali wamekuwa wakianzisha biashara bila mpango wa biashara. Mpango wa biashara ni namna ya kuweza kuona kwa jinsi gani biashara itafanyika. Mpango wa biashara hutoa mwelekeo kwa mjasiriamali kujua bidhaa atakazouza, soko lake, gharama, mahitaji pamoja na fedha zitakazohitajika katika biashara husika, matokeo tarajiwa ya biashara na kadhalika. Ni namna ya kujitengenezea mwelekeo katika biashara. Bila mpango wa biashara, unaweza kujikuta unafanya biashara ambayo haina mwelekeo wowote, zaidi ya kununua mali kwa bei ya chini na kuuza kwa bei ya juu, wakati kuna gharama mbalimbali za kuzingatia katika biashara yako. Biashara yoyote ili ipate mafanikio inafaa kuwa na mpango wa biashara utakaotoa mwelekeo wa wapi biashara ielekee na kutoa matokeo gani.

2. Matumizi mabaya ya pesa

Epuka gharama zisizo za lazima. Zipo biashara ambazo hazifanyi vizuri kutokana na wajasiriamali kuingia katika gharama ambazo wangeweza kuacha. Kuna wajasiriamali ambao hawajali kabisa gharama ndogo kwa kuwa ni ndogo Wajasiriamali wanapaswa wakumbuke kuwa gharama ndogo husababisha baadaye kupatikana gharama kubwa kwa ujumla wake. Jaribu kuandika gharama mbalimbali unazoingia katika biashara na baadae utagundua nyingine si za lazima. Kuepuka kupata matatizo, yafaa kutenganisha matumizi ya fedha kwa ajili ya biashara na matumizi binafsi. Bila kutenganisha matumizi ya biashara na binafsi biashara haiwezi kuendelea hata kama ulianza na mtaji mkubwa kiasi gani, utashindwa tu baadae. Usichanganye matumizi binafsi na biashara. Wewe kama mmiliki wa biashara yako inafaa ujijengee nidhamu ya uendeshaji, na hasa nidhamu ya matumizi ya fedha.

3. Kutojiwekea malengo katika biashara

Jiulize nini malengo ya hicho unachokifanya? Kwa nini umeamua kufanya biashara fulani na si nyinginezo? Kuwa na malengo ni jambo la msingi katika kujenga mafanikio unayotamani. Usifanye mambo kwa kuona tu fulani kafanikiwa. Wapo wajasiriamali ambao wamejiingiza kwenye biashara ya mbalimbali kwa sababu tu wamesikia biashara fulani inalipa sio zaidi ya hapo. Lazima kufanya biashara kwa malengo na hasa malengo utakayoweza kuyasimamia.

4. Kutokuweka kumbukumbu za biashara

Biashara yako huenda ikawa haifanyi vizuri kutokana na kutokuwa na namna ya kutunza kumbukumbu za biashara. Kumbuka mali bila daftari hupotea bila habari. Kama hutunzi kumbukumbu za biashara unategemea kupata matokeo gani? Ni muhimu kwako mjasiriamali kujiwekea utaratibu mzuri wa kutunza kumbukumbu za biashara yako. Mjasiriamali anatakiwa aonyeshe mchanganuo wa mali zilizonunuliwa kwa kutenganisha aina za bidhaa na gharama zake. Katika bidhaa ulizonunua kwa ajili ya biashara yako yafaa utengeneze mchanganuo wa namna bora ya kutunza kumbukumbu. Usitembee na kumbukumbu za biashara zako kichwani kwani wewe ni binadamu huwezi kuyakumbuka matukio yote .

5. Kutokujua eneo sahihi la kufanyia biashara

Ili kuepuka biashara kufanya vibaya ni lazima utambue eneo la biashara yako, jiulize je biashara yako iko katika eneo sahihi? Kuna wajasiriamali wamekwama kwenye biashara zao kwa sababu tu wameweka biashara katika maeneo ambayo si sahihi. Kama mjasiriamali yafaa kuchagua eneo la biashara kutokana na biashara yako, na si urahisi wa upatikanaji wa eneo ndio usababishe wewe kuchagua eneo husika.

Tambua; ili uweze kuepuka matatizo ya kutofanya vizuri kwa biashara yako yafaa kujipima juu ya uwezo wako wa kibiashara na uzoefu katika biashara husika. Fanya biashara ambayo unaiweza, usiige au kufuata mkumbo toka kwa wengine. TUPO PAMOJA

Makala hii imeandikwa na Geofrey Mwakatika, Unaweza kutembelea blog yake Geofrey Mwakatika kujifunza zaidi.