Kuna wakati huwa tunaishi bila kujua ni kwa nini tunafanya au hatufanyi mambo Fulani. Hebu jiulize, ni kwa nini wengine wanapigana na kuuana kwa sababu ya fedha, kwa sababu ya kutaka mali au kwa sababu ya kutaka sifa, wakati kwa wengine, hayo ni masuala madogo? Hiyo yote huwa inatokana na binadamu kuhitaji kufikia kiwango fulani cha juu cha ridhiko katika maisha yake. Kutokana na watu wengi kutafuta kuridhika huko katika maisha yao hujikuta wakifanya kila linalowezezekana ili kuweza kutimiza lengo hilo hata kama kutafuta pesa kwa njia zisizo za halali ili mradi tu mioyo yao itulie na kupata ridhiko wanalolitaka.

Kuridhika ni kitu ambacho kimekuwa kinawatesa wengi bila kujijua, ndio maana wengi hujikuta wakifanya mambo ya ajabu ikiwemo kujihusisha hata na kunywa pombe kama njia ya kutafuta ridhiko katika maisha yao. Inawezekana hata wewe umekiwa ukiteswa na kitu hiki mara nyingi kwa namna moja au nyingine na kujiuliza kwa nini iko hivi bila kupata majibu.Kitu wasichokijua au kwa bahati mbaya watu wengi huwa hawajui kwamba hadi kufikia ridhiko halisi, kuna hatua anazotakiwa kupitia mtu nikiwa na maana kwamba ni kitu ambacho hakiji tu. 
Hatua hizi huwa ni lazima kila mmoja aweze kuzifikia ili aweze kupata ridhiko halisi ambalo wengi wanalitafuta katika maisha yao, vinginevyo bila kupitia hatua hizo maisha yote itakuwa ni kuhangaika tu, kutafuta ridhiko na utajikuta huwezi kufikia. Hii ndio huwa sababu hasa utasikia wengine wakisema ‘Aaah binadamu hawaridhiki siku zote’ ni kutokana na kutokujua hatua muhimu za kutafuta ridhiko. Bila kufikia ngazi au hatua hizo ni ngumu sana kuridhika katika maisha yako ndio maana unakuta kuna mtu ana pesa lakini hana furaha. Ngazi hizi wanasaikolojia huziita ngazi za mahitaji ambazo huanzia chini kabisa kama hivi:-
1. Ngazi ya mahitaji ya kimwili.
Hii huwa ni ngazi ya chini kabisa ambayo hujihusisha hasa na vitu kama vile chakula, maji, mavazi na malazi. Hapa ni mwili, ambao ndiyo unamhangaisha mtu. Mtu anatafuta kula, kuvaa na kulala. Kama mtu akishindwa kuridhika kwenye ngazi hii, ni vigumu sana kupanda katika ngazi ya pili, ambayo itasaidia kumpandisha kwenda ngazi za juu kuelekea ridhiko lililo kamili. Watu wengi kwa bahati mbaya, hata kwenye ngazi hii huwa hawavuki. Hujikuta ni watu unapokutana nao wanakwambia wanatafuta pesa ya kula hii yote inaonyesha kuwa wapo bado katika ngazi ya kwanza kabisa. Kushindwa kuridhika au kumudu katika hali hii hupelekea kuleta matatizo mengi katika jamii ikiwemo masuala ya wizi wa namna tofauti unaoujua, hivyo hii ni ngazi muhimu sana kuipita.
 
 
2. Ngazi ya usalama.
Hii huwa ni ngazi ya pili kuelekea kwenye ridhiko unalolihitaji katika maisha yako. Mara nyingi mtu aliyeridhika katika ngazi ya kwanza, hujikuta akitafuta usalama, uhakika wa usalama wake na ulinzi. Hapa ndipo mtu pale anapotafuta kumiliki silaha labda, anaweka mageti mazito kwenye nyumba yake. Lakini pia anaweza kufanya au kuchukua hatua nyingine mbalimbali za kutafuta usalama wake. Kama mtu hajaridhika kwenye hatua ya ngazi ya awali, ni vigumu sana kwake kufikiria kuhusu usalama wake. Mtu mwenye njaa anakuwa yupo tayari kuhatarisha maisha yake kwa kuiba. Ni kama vile haiwezekani kumwambia ajali usalama wake, kwani kuruka ngazi za mahitaji ni vigumu.
Mtu ambaye amefungwa na kula mapochopocho, ambaye bado anahangaika kwenye ngazi ya kwanza ya mahitaji, hawezi kujali kuhusu usalama wa afya yake. Mtu ambaye akiwa hajaridhika kwenye ngazi moja hawezi kuvuka kwenda ngazi nyingine. Anapojaribu kufanya hivyo ni lazima aumie. Kuna watu wanaokufa au kuuwana kwa sababu ya fedha, kwa sababu ya chakula, sababu ya wanaume au wanawake au kwa sababu ya mirathi. Hawa ni watu wanaoishi kwenye ngazi ya awali ya kuelekea kwenye ridhiko la kweli. Huuwana kwa sababu hawajamudu kuingia katika ngazi ya pili ya usalama. Tunapofungwa na njaa hatuwezi kujali usalama wetu.
3. Ngazi ya kupendwa.
Kila binadamu hutamani kuuona wengine wanamkubali, kumpenda au kuunda umoja au ukaribu na wengine. Hapo ndipo pale ambapo mtu anajiunga na jumuiya, anakuwa na marafiki au jambo ama mahali ambapo anakutana na wengine. Ni vigumu kwa mtu au watu  ambao hawana uhakika wa usalama wao, kujali kuhusu kukubaliwa na wengine. Baada ya mtu kuhakikisha kwamba yu salama ndipo anapoweza kufikiria kukubaliwa, kupendwa na kupokelewa na wengine.
4. Ngazi ya utambuzi kamili.
Hii ni ngazi ambayo unaweza kutambuliwa na watu au kutambua wengine kama viumbe wenye uwezo na wanaomudu. Hii ni hatua ya juu hata hivyo, kwani inahusisha kujiamini, ambako wengi hawana. Kama mtu hajaridhika katika zile hatua za awali, ni wazi kabisa atashindwa kujiamini. Kujiamini ni mtu kujikubali na kukabiliana na maisha anayoishi. Unapokuwa katika hatua hii unakuwa upo kwenye utambuzi. Hatua hii ni ya binadamu kuweza kutambua uwezo mkubwa alionao binadamu. Katika hatua hii, ndipo binadamu anapata uwezo wa kufanya makubwa ya kutengeneza na siyo ya kubomoa kwenye maisha. 
Ni vigumu kutegemea mtu ambaye hajaridhika kwenye ngazi za chini za mahitaji ya binadamu kupata ridhiko la kweli. Ili mtu apate ridhiko la kweli kwenye maisha yake, ni lazima ahakikishe kwamba, mahitaji kuanzia ngazi ya kwanza hadi ya nne yanamridhisha. Ni sisi tunaoamua kuridhika, siyo vile vinavyotuzunguka. Ndio maana unaweza kukuta mtu mwenye fedha nyingi, elimu kubwa na umaarufu, anakunywa pombe hadi anabebwa kwenye mkokoteni. Huyu hajali kuhusu usalama wake, heshima yake au kingine, kwa sababu ni vigumu kwetu kama binadamu kuvuka nguvu za mahitaji. 
Ili nasi tuweze kufikia mahali ambapo tutaweza kutumia nguvu kubwa tulizonazo katika kufikia ridhiko na hatimaye kukifanya kile kilichotuleta duniani, hatuna budi kukagua kila ngazi. Je, ngazi ya kwanza tumeimudu, ya pili, ya tatu na ya nne? Bahati mbaya moja kubwa kwenye suala hili ni kwamba, wengi wetu huishia kwenye ngazi ya kwanza ya mahitaji ya binadamu. Ni muhimu kuwa makini katika kila hatua, kama kweli unataka kufikia ridhiko kamili.
Nakutakia ushindi katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea AMKA MTANZANIA  kwa kujifunza na kuhamasika zaidi.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE.
IMANI NGWANGWALU
0767 04 80 35/ingwangwalu@gmail.com