Muda mwingine unaweza ukajiuliza kwa nini mteja au wateja Fulani siku hizi huwaoni katika biashara yako, unaanza kumtafuta mchawi ni nani katika biashara yako kumbe mchawi ni wewe mwenyewe ambaye unaweza ukawavuta wateja wengi au mteja au ukaongeza mteja ,wateja katika biashara yako hii inatokana tu na jinsi gani unatoa huduma yako na kumhudumia mteja pia.
Leo tutaangalia ni sababu gani ambazo zinaweza kusababisha kumpoteza au kumkera mteja wako nazo ni;
1. Kuchelewa Kufungua Biashara
Kuna baadhi ya wamiliki wa biashara wanachelewa kufungua biashara na unakuta mteja anahitajia kupata huduma mapema ukilinganisha na muda wako ambao unafungua biashara sababu hii inaweza ikampoteza mteja au kumkera kama tabia yako wewe kila siku ni kuchelewa mteja anakusubiri katika eneo la biashara badala ya wewe kumsubiri mteja sababu inaweza ikapelekea kumkera au kumpoteza mteja wako. 

 
2. Kufanya Biashara kwa Mazoea/ Kujisikia
Unapokuwa umeamua kufanya biashara basi fanya kila siku bila mazoea au kujisikia kuna wafanyabiashara wengine wanafanya biashara kwa kujisikia au kwa mazoea kwa mfano, leo anaweza kufungua kesho kafunga sasa tabia kama hii inaweza kumsababishia mteja kupata kero na kukuhama kabisa ukiamua kufanya biashara fanya kila siku bila kukata tama bila kujali siku yaani siku Fulani kuna wateja na siku Fulani hakuna wateja hivyo basi unaamua kutofanya biashara kwa hiyo acha kufanya biashara kwa mazoea.
SOMA; Kufanikiwa, Jua Kitu Ambacho Wengine Hawajui, Ila Usiwe Mchoyo.
3. Kuacha Biashara peke yake
Kuna tabia ya wafanyabiashara wanaweza kufungua biashara yao na kuacha peke yake anazungukazunguka au kwenda sehemu kupiga stori huku akiacha biashara yake wazi mteja akija anapata shida ya kumtafuta mtoa huduma unafikiri kama kuna sehemu nyingine ambapo mteja huyu anaenda na kumkuta mtoa huduma yuko katika eneo lake la biashara kila siku je ataweza kushawishika tena kurudi kwako? Kama sehemu nyingine anahudumiwa vizuri?
4. Kuwa na Lugha/Kauli mbaya
Unapokuwa unafanya biashara unatakiwa uwe na kauli nzuri ambazo zitamvutia mteja kuja kwako kupata huduma. Kuna wateja wengine ndio wanaweza kuwa na kauli mbaya lakini wewe hupaswi kuwa na kauli mbaya hupaswi kumjibu kwa lugha mbaya soma saikolojia ya mteja au wateja wako muudumie kwa upendo, kwa ukarimu wa hali ya juu ili siku nyingine arudi tena kwako. Kwa hiyo kauli mbaya ni moja ya sababu ambazo zinaweza kukuletea matokeo hasi katika biashara yako. Chunga sana ulimi wako katika biashara.
5. Kutopenda Biashara yako
Kuna wafanyabiashara wengine wanatoa huduma kama vile wamelazimishwa kufanya biashara hiyo. Kutopenda kazi yako ni moja sababu zitakozomfanya mteja naye asivutiwe na biashara yako. Kuwa na uso wa furaha mchangamkie mteja ongea naye vema katika lugha ya ushawishi onesha jinsi gani unaipenda kazi yako, unafanya kwa moyo na juhudi zote huwezi kumpoteza mteja wako. Kwa hiyo ili ufanikiwe katika jambo Fulani penda kwanza hicho unachokifanya kwa moyo wote.
6. Kubadilisha bei mara kwa mara.
Katika kila bidhaa unayouza mfano duka kuna kuwa na bei elekezi ya vitu unavyouza kwa bei ya jumla au rejareja. Sasa kuna baadhi ya wafanyabiashara wanauza kwa bei ya juu sana ili kupata faida ya juu hapa unakuwa unamlangua mteja na kumkatisha tamaa tena ya kurudi kwako kupata huduma, kwa hiyo unapofanya biashara usiwe mtu wa kubadilisha bei mara kwa mara leo mteja akija bei nyingine kesho bei nyingine itamfanya akose imani na wewe na kukukimbia kabisa.
SOMA; Sababu Tano(5) Binafsi Zinazorudisha Biashara Za Kitanzania Nyuma.
Hivyo basi, ziko sababu nyingine na hizo ni baadhi tu ya sababu ambazo zinaweza kuwa kero au kumpoteza mteja katika biashara yako. Kama wewe ni mfanyabiashara na una tabia kama hizi chukua hatua mara moja.
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com