Hakuna mtu ambaye hapendi kuongeza kipato chake, iwe ameajiriwa au amejiajiri mwenyewe. Na sheria ya kipato ni kwamba inabidi kiongezeke kwa sababu kadiri siku zinavyokwenda gharama za maisha zinaongezeka na hata mfumuko wa bei unapunguza thamani ya fedha. Milioni moja ya miaka mitano iliyopita, siyo sawa na milioni moja ya mwaka huu.
Pamoja na umuhimu wa kuongeza kipato, bado watu wengi hawajui njia sahihi ya kuongeza kipato. Na hii ni kwa sababu hakuna sehemu ambapo somo la kuongeza kipato linafundishwa moja kwa moja. Badala yake tunaangalia wengine wanafanya nini ili kuongeza kipato chao na sisi tunaiga.
Kuna njia nyingi sana ambazo watu wamekuwa wakitumia kuongeza vipato vyao, lakini njia hizi sio bora na zimekuwa haziwapatii kile kipato ambacho wanakitaka kweli. Leo kupitia makala hii tutakwenda kujifunza njia bora sana ya kujiongezea kipato chako ambayo kama ukianza kuitumia sasa utakwenda juu zaidi kwenye kipato.
Lakini kabla hatujaangalia ni njia ipi bora, kwanza tuanze kwa kupitia njia zilizozoeleka ambazo hazileti matunda bora.

 
Njia za kuongeza kipato kwa waajiriwa, ambazo hazizai matunda bora.
Kwa waajiriwa, swala la kuongezewa kipato lina changamoto nyingi sana. Hii ni kwa sababu sio wao wenyewe wanaoamua moja kwa moja ni kiasi gani walipwe. Na hivyo kuna baadhi ya njia ambazo waajiriwa wamekuwa wakizituma kutaka kuongeza kipato chao. Japo njia hizi zimekuwa hazizai matunda, bado wamekuwa wakizing’ang’ania. Hizi hapa ni baadhi ya njia hizo;
1. Kudai kuongezwa kipato. Hapa waajiriwa huja na madai ya kuongezewa kipato na kuwataka waajiri wao wawaongeze kipato.
2. Kugoma na kushinikiza. Ikiwa waajiriwa hawatakubali mapendekezo, waajiriwa huwa wanagoma na kushinikiza kuongezewa kipato.
3. Kufanya kazi kwa kiwango cha chini, hawa waajiriwa hufikiri kwamba kwa kuwa kipato ni kidogo, basi na wao wafanye kazi ndogo, japo hii ni njia mbovu zaidi.
4. Kuiba na kupokea rushwa. Kwa kuwa kipato hakitoshelezi, basi waajiriwa huamua ‘kujiongeza’ ili waweze kukidhi mahitaji yao. Na hapa hujiingiza kwenye vitendo vya wizi, ubadhilifu au rushwa. Njia hii pia ina madhara makubwa zaidi mbeleni.
Hizi ni baadhi ya njia ambazo waajiriwa wamekuwa wakitumia kutaka kuongeza kipato chao. Lakini njia zote hizi sio za uhakika na zimepelekea hali kuwa mbaya zaidi ya ilivyokuwa awali.
SOMA; FEDHA: Hivi Ndivyo Unavyoweza Kumudu Kujiongezea Kipato Chako Kwa Kutumia Njia Hizi Rahisi.
Njia za kuongeza kipato kwa waliojiajiri na wanaofanya biashara ambazo hazizai matunda.
Waliojiajiri pia na wao wamekuwa wakifanya jitihada za kujiongezea kipato. Japo pia wamekuwa wakitumia njia ambazo haziwaletei matunda mazuri. Hapa tutaziangalia baadhi ya njia wanazotumia kuongeza vipato vyao.
1. Kuongeza bei ya bidhaa au huduma zao ili tu kupata faida kubwa. Hii inaweza kuongeza kipato kwa muda mfupi lakini baadaye inaleta madhara.
2. Kuwalipa kidogo wale wanaowasaidia kwenye shughuli zao. Hii pia haina matunda mazuri kwa siku za mbeleni.
3. Kulangua na kutapeli. Hapa baadhi ya watu wanawashawishi watu wanunue wakijua kabisa haiendi kuwasaidia, na hapa kuzidi kuharibu biashara zao.
4. Kufanya kinyume na sheria, njia hii pia hufika mwisho pale ambapo wanagundulika na kupelekea biashara kufa kabisa.
Hizi ndizo njia ambazo watu wanapenda kuzitumia kuongeza kipato chao. Lakini cha kusikitisha ni kwamba njia hizi hazileti kipato cha uhakika, lakini bado watu wanapenda kuzitumia. Unajua ni kwa nini? Nitakueleza mwishoni, kwanza tuangalie njia bora ya kujiongezea kipato.
Njia bora na ya uhakika ya kujiongezea kipato chako.
Tumeshaona njia ambazo siyo bora na ambazo wengi wanapenda kuzitumia. Sasa tuone ni ipi njia bora, ambayo hata wewe ukianza kuitumia utapata matokeo bora.
Njia bora na ya uhakika ya kuongeza kipati ni wewe KUONGEZA THAMANI ya kile unachotoa au unachofanya. Ni hivyo tu, iwe umeajiriwa au umejiajiri au unafanya biashara. Kadiri unavyoongeza thamani ya kile unachotoa ndivyo unavyojihakikishia kupata kipato kikubwa zaidi.
Kama umeajiriwa ongeza thamani ya kazi unayofanya, weka ubora zaidi, jitume na ongeza ufanisi wako na uzalishaji wako. Usiangalie ni kiasi gani unalipwa, au wengine wanafanya nini. Unachohitaji kufanya ni kuongeza thamani, weka thamani kubwa ambapo yule anayepokea unachofanya, anaona hiki ni bora sana. Unapofanya hivi kwa muda mrefu ndivyo unavyojiweka kwenye mazingira ya kupata kipato kikubwa zaidi, kwa sababu thamani yako pia itaongezeka na hata kama mwajiri wako wa sasa hatakuongeza kipato, utaziona fursa nyingi za kuongeza kipato.
SOMA; Tengeneza Kipato Cha Ziada Huku Ukiendelea Kufanya Unachofanya Sasa.
Kwa waliojiajiri na wafanyabiashara, ongeza thamani kwa wateja wako. Kwa bidhaa na huduma unayotoa, hakikisha ina thamani kubwa, na inakwenda kumsaidia kweli yule ambaye anainunua. Wajali sana wateja wako kwa kuhakikisha wanapata kilicho bora. Jua matatizo yao ni yapi na biashara yako inawezaje kuyatatua. Kwa njia hii utawapa thamani kubwa na wao watakuwa wa kwanza kuitangaza biashara yako na hivyo kukuongezea wateja wengi zaidi.
Je ni njia ipi ya kwanza kabisa unayoweza kutumia kuongeza thamani kwa wale wanaotegemea unachofanya?
Njia hii ni kujua jinsi ya kutoa huduma bora kwa wateja wako. Kwa wote walioajiriwa na waliojiajiri, una mteja, na kadiri unavyompatia mteja wako huduma bora kabisa, ndivyo unavyojiweka kwenye nafasi ya kuongeza kipato chako. Na ndiyo maana tumeandaa semina kwa njia ya mtandao inayohusu UTOAJI WA HUDUMA BORA SANA KWA WATEJA. Semina hii itaendeshwa kwa njia ya wasap na email na gharama za kushiriki semina hii ni tsh elfu 20. Kama utapenda kushiriki semina hii ili ujifunze mbinu hizi na uwezekuongeza kipato chako, andika ujumbe wa SEMINA HUDUMA KWA WATEJA kwenda namba 0717396253, ujumbe utume kwenye wasap kisha nitakuweka kwenye kundi la semina. Karibu sana.
Swali la mwisho, kwa nini watu hawapendi kutumia njia hii ya uhakika ya kuongeza kipato?
Kwa sababu siyo njia rahisi, unajua watu wanapenda vitu ambavyo ni rahisi, hawataki kujichosha na hivyo hukimbilia vile ambavyo siyo vigumu. Kugoma au kuchukua rushwa ni rahisi na haikuhitaji uweke juhudi za ziada. Ila kuongeza thamani kwenye kile unachofanya, unahitaji juhudi na maarifa ya ziada, kama hivi ambavyo unahitaji ujifunze kwenye semina hii ya huduma kwa wateja.
Lakini ugumu huu unalipa, kama ambavyo wote tunajua, vitu vigumu vina thamani kubwa sana baadaye na vitu rahisi huwa havidumu. Hivyo nakusihi sana kama rafiki yangu, tumia njia hii ya kuongeza thamani, na ili uwe vizuri zaidi, karibu tushiriki pamoja semina ya huduma kwa wateja. Tuma ujumbe kwa njia ya wasap kwenye namba 0717396253. Karibu sana.
Nakutakia kila la kheri katika kuongeza thamani kwenye kile unachofanya ili uweze kuongeza kipato chako.
TUPO PAMOJA,
Rafiki na Kocha wako,
Makirita Amani,
makirita@kisimachamaarifa.co.tz