Mara nyingi si kitu cha kushangaza wengi wetu tunapoanza kazi zetu, ziwe za kuajiriwa au kujiajiri huwa tunaanza kwa hamasa kubwa sana. Lakini hata hivyo kwa bahati mbaya hamasa hiyo huwa haidumu sana kwa walio wengi. Hiyo ikiwa na maana kwamba kwa kadri siku zinavyokwenda hamasa ambayo wengi wanakuwa wameanza nayo kwenye kazi zao,  inakuwa inapungua kidogo kidogo.
Jambo la kujiuliza mimi na wewe ni kwanini hamasa hii huwa haidumu sana. Ni kitu gani ambacho hukosekana na kupelekea watu kufanya kazi kwa kujisukuma sana kutokana na kukosa hamasa hiyo? Unaweza ukawa hujui hilo sana, lakini kwa kusoma makala haya, naamini utapata majibu kamili. Hebu tuangazie nukta kadhaa za kutusaidia kujua kwanini hamasa hupotea kwenye kazi au kwa kile tunachokifanya?  
1. Kushindwa kupata matokeo unayoyataka.
Mara nyingi tunapoanza kazi fulani huwa tunakuwa ni watu wa kutegemea matarajio ya aina fulani. Huwa ni watu ambao tunakuwa tumejipa matumaini kwa kazi hii nikiifanya itanipa mafaniko haya na haya. Tunapoanza kufanya kazi hiyo na kushindwa kupata kile tunachokitegemea kukata tamaa na kukosa hamasa huanza kujitokeza.
Hebu jaribu kuangalia ile kazi ambayo ulipoanza kuifanya uliianza kwa mategemeo makubwa. Kwa mfano pengine uliambiwa utalipwa mshahara mkubwa, lakini matokeo yake hukulipwa mshahara huo kama ulivyotegemea. Naamini kilichokukuta baada ya kukosa kile ulichokuwa ukikitegemea ni kupungua kwa hamasa. Wengi hali hiii huwa huwatokea hivyo na kujikuta huharibu zaidi kazi zao kutokana na kukosa matumaini ya mwanzo.
Kitu cha kufanya.
Unapoanza kazi au jambo lolote, anza kwa matumaini makubwa lakini mambo yanapoenda hovyo usikukabali ukakosa hamasa au kukatishwa tamaa. Jifunze hili kwa kutambua kwamba maisha yana pande mbili.
 2. Kukosa maono.
Kitu chochote unapoanza kukifanya hakikisha unakifanya huku ukiwa na maono makubwa makubwa. Ni lazima ujue mimi kwa kufanya jambo hili baada ya mwaka mmoja au miaka miwili mbele nitakuwa hapa au pale. Inapotokea ukafanya jambo halafu ukawa huna maono yanayo fanana na kitu ninachoeleza hapa, elewa kabisa ikitokea changamoto yoyote mbele yako, kukosa hamasa inakuwa ni rahisi sana kwako. Unapokuwa una maono yanakuwa yanakusaidia kuvuka milima na mabonde ya kila kinachokuzuia kufanikiwa na hutakubali kukosa hamsa.
Kwa mfano ukiangalia watu wengi ambao wanakosa hamasa kwenye kazi zao mara nyingi hawana maono. Hebu jaribu kuangalia watu ambao wameajiriwa kwenye kampuni fulani, wengi wa wafanyakazi hukosa hamasa kwa sababu ya kutokuwa na maono. Ukiwa na maono unajua kazi yako itakunufaisha vipi, ni lazima hamasa uwe nayo na ukiikosa upo tayari hata kuitafuta chini ya uvungu wa kitanda uipate kama kweli imejificha huko.
Kitu cha kufanya.
Hakikisha una maono sahihi ya kile unachokifanya, hiyo itakusaidia kujitengenezea hamasa ya kudumu karibu siku zote.
3. Kuzoea kazi.
Kama unafanya kazi zako kwa mazoea na kusahau kuweka juhudi za kuboresha, tambua ni rajhisi kuweza kupoteza hamasa. Kazi yoyote unayoifanya kama unataka ikupe hamasa ijengee utaratibu wa kuifanya kwa kutokuipa mazoea. Ifanye kazi yako kwa ufanisi na upya zaidi, utajenga hamasa.
Kumbuka siku zote, mazoea katika kazi ni kitu kibaya sana. ili uweze kufanikiwa hutakiwi kujenga mazoea na kitu chochote. Kila kitu kipe uzito sawa kwa kukiona ni cha muhimu wakati wote. Hata mafanikio ukiyapata halafu ukaanza kujifanya unayozea utajikuta unayopoteza kwa sababu tu ya mazoea, utakuwa ukiyafanya mambo kwa ukawaida sana.
Kitu cha kufanya.
Jifunze kila wakati kutokuwa na mazoea na kazi unayoifanya iwe yako au ya kuajiriwa. Kwa kuchukua hatua hiyo itakujengea nidhamu ya hali ya juu itakayokufanya uwe na hamasa muda mwingi.
 4. Kukosa ushirikiano.
Kwa kawaida unapofanya kazi ya aina fulani halafu ukakosa ushirikiano mkubwa na wale wanaokusaidia, hakuna ubishi mara nyingi hamasa huwa inapungua sana au kutoweka kabisa. ni kitu ambacho huwatesa wengi na kuwafanya waone wamekosea kufanya kitu hicho na watu hao. Kwa kuwaza hivyo hupelekea hamasa kupungua siku hadi siku.
Naamini mpaka hapo umejifunza na umetambua mambo ynayoweza kukusababishia ukakosa hamasa kwenye kazi unayoifanya. Najua pia zipo sababu nyingi ambazo hupelekea kwa watu kukosa hamasa kwenye kile wanachokifanya. Lakini kwa kupitia makala hii nimekupa baaadhi ya sababu ziwe kama msingi wa kukusidia kutokukata tamaa.
AMKA MTANZANIA inakutakia siku njema na kila la kheri katika kufikia mafanikio makubwa.
Kwa makala nyingine za maisha na mafanikio tembelea pia DIRA YA MAFANIKIO kuweza kujifunza kila siku.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki,
Imani Ngwangwalu,
Simu; 0713 048035,