Hakuna siri kwenye mafanikio, ila endelea kusoma kwa sababu yale utakayojifunza siyo uliyozoea kuyasikia kwenye maisha ya kawaida.

Ni mambo yaliyo wazi kabisa, lakini yamekuwa hayazungumziwi wazi, na ndiyo maana yamekuwa yanaitwa siri.

Ukiwachukua watu 100 kutoka eneo lolote lile, kumi watakuwa na mafanikio makubwa kuliko 90 na mmoja kati yao atakuwa na mafanikio makubwa kuliko wote.

Ni namba hizi ndiyo zimekuwa zinawachanganya watu, wasielewe kwa nini wachache sana ndiyo wafanikiwe huku wengi wanaopenda kufanikiwa wakiwa hawafanikiwi.

Kiu ya kutaka kupata siri za mafanikio siyo ya zama hizi tunazoishi, imekuwepo tangu enzi na enzi.

siri ya mafanikio.jpg

Mwaka 1912 mwandishi Orison Swett Marden alikusanya pamoja ushuhuda wa wale waliofanikiwa, kwa namna walivyoeleza wao wenyewe na kuja na kitabu alichokiita; How They Succeeded: Life Stories of Successful Men Told by Themselves. Kitabu hicho kimesheheni hadithi za watu waliokuwa na mafanikio makubwa sana kipindi hicho, kwa namna ambavyo walieleza wenyewe.

Ni kitu kimoja kusoma hadithi ya mafanikio ya mtu inayoelezwa na wengine na ni kitu kingine tofauti kabisa kusoma hadithi hiyo ikielezwa na mtu mwenyewe.

Upekee wa kitabu hiki, unatufanya tuwasikie wenyewe wanasemaje kuhusu mafanikio yao.

Mmoja wa watu waliofanikiwa ambaye hadithi yake inapatikana kwenye kitabu hiki ni aliyekuwa mwandishi Amelia E. Barr (March 29, 1831–March 10, 1919). Ambaye pamoja na kupoteza mume wake pamoja na watoto wake watatu kati ya sita aliokuwa nao, aliweza kufikia mafanikio makubwa sana kwenye uandishi.

Kwenye insha yake iliyo kwenye kitabu hiki, ameshirikisha siri 9 za mafanikio kutokana na uzoefu wake binafsi.

Hapa tunakwenda kujifunza siri hizo kama alivyoeleza mwenyewe, kisha nitaongeza hatua ya wewe kuchukua ili kuweza kufanikiwa sana.

Moja; kuwa tayari kwa maumivu.

Amelia; watu wanafanikiwa kwa sababu wako tayari kupokea maumivu wanayopitia ili kufanikiwa. Juhudi na uvumilivu ni muhimu na wote waliofanikiwa walifanya maamuzi na kung’ang’ana nayo. Wanajua kusudi lao na wanafanya maamuzi ya kulifikia.

Somo; jua hasa nini unachotaka kwenye maisha yako, amua kwamba utapata kitu hicho na chukua hatua kukipata. Usikate tamaa hata kama unapitia maumivu makali kiasi gani, hakuna aliyewahi kufanikiwa bila ya kupitia maumivu.

SOMA; Njia Ya Uhakika Ya Kupata Utajiri Bila Kutegemea Bahati.

Mbili; weka kazi kila siku.

Amelia; mafanikio ni zawadi kwa wale ambao wanaweka kazi kila siku. Hii ndiyo siri kuu ya mafanikio, kuweka juhudi kuliko wengine wanavyoweka. Kama kuna kitu hujui, utajifunza kwa kufanya. Na hata pale unapopata matokeo usiyotegemea, usiache kuweka juhudi mpaka umepata unachotaka.

Somo; weka kazi kila siku, siyo pale unapojisikia, au pale wengine wanapofanya, bali wewe unapaswa kuweka kazi kila siku. Hakuna mafanikio bila ya kuweka kazi, usidanganywe na wale wanaokuambia mafanikio yanahitaji kufanya kazi kwa akili siyo kwa nguvu, wewe weka nguvu na akili kwenye kazi na utafanikiwa.

Tatu; usisumbuke na wanaokupinga.

Amelia; safari yako ya mafanikio haitakuwa rahisi, utakutana na vikwazo na moja ya vikwazo hivyo ni watu watakaochagua kuwa maadui wako na kukupinga kwenye kile unachofanya. Usiumizwe na upingaji wa wale wanaokupinga, badala yake utumie kupiga hatua zaidi. Ukinzani una nguvu ya kukusukuma zaidi.

Somo; usitegemee kila mtu akubaliane na wewe, wengi watakupinga, kukukosoa na kukukatisha tamaa. Lakini kumbuka kitu hiki kimoja, wote hao hawajui nini unataka na uko tayari kujitoa kiasi gani kukipata. Hivyo usiumizwe na ukosoaji wao, kama kuna kitu chenye manufaa wanakigusia kifanyie kazi, kama hakuna wapuuze na endelea na safari yako.

Nne; bahati inauzwa.

Amelia; kosa kubwa kwenye mafanikio ni kufikiria kwamba ni jambo la bahati, kwamba wanaofanikiwa wanakuwa wamepata bahati. Dunia inaendeshwa na sheria kali ambazo hazitoi nafasi kubwa kwa bahati kufanya kazi. Asili huwa inauza vitu vyake, huwa haivitoi bure, hivyo hata bahati, utainunua, hutapewa bure.

Somo; ni kweli waliofanikiwa wanakutana na bahati fulani, lakini bahati hizo huwa haziwafuati wakiwa wamelala kitandani, bali zinawakuta wakiwa wanaweka kazi kwenye kile wanachotaka. Hivyo kama unataka kukutana na bahati, lazima ulipe gharama ya kuwa tayari kuweka kazi. Kama ambavyo tumekuwa tunajifunza, bahati ni pale maandalizi yanapokutana na fursa.

Tano; pasha chuma moto.

Amelia; kwa miaka tumekuwa tunaambiwa tuziangalie fursa, kupiga wakati chuma ni cha moto. Ni vizuri, lakini itakuwa bora kama tutakifanya chuma kuwa cha moto kwa kupiga, badala ya kusubiri chuma kiwe cha moto ndiyo tupige.

Somo; usisubiri mpaka fursa ije ndiyo uanze kuchukua hatua, badala yake anza kuchukua hatua na utakutana na fursa. Ukiwa kwenye kuchukua hatua inakuwa rahisi kuziona na kuzitumia fursa kuliko ukiwa unasubiria mpaka fursa ije huku hauchukui hatua. Usisubiri chuma kiwe cha moto ndiyo upige, kipige chuma mpaka kiwe cha moto.

Sita; unahitaji muda.

Amelia; kila kitu kizuri kinahitaji muda, usiwe na haraka kwenye kazi yako. Weka muda na zama ndani kwenye kazi yako, kadiri unavyoweka muda zaidi ndivyo inavyokulipa zaidi. Kazi za hovyo hufanywa kwa haraka, akili kubwa ni kujipa muda wa kufanya vizuri kile ambacho wengine wanafanya vibaya.

Somo; hakuna njia ya mkato ya kufikia mafanikio makubwa, yeyote anayekuambia njia hiyo ipo anataka kukutapeli. Jipe muda, kama ukiwahi sana jua itakuchukua miaka 10, lakini mara nyingi ni zaidi ya hapo. Acha papara za kutaka mafanikio ya haraka, hayapo. Jipe muda, weka muda wa kutosha kwenye kazi yako, jua kwa kina kile unachokifanya na kazana kuwa bora, kila unachoweka kitakulipa zaidi.

SOMA; Huu Ndiyo Msingi Mkuu Wa Maisha Ya Mafanikio Unaopaswa Kuujua Na Kuuishi Kila Siku.

Saba; kuwa na mpangilio.

Amelia; kazi inayofanywa bila mpangilio siyo kazi nzuri, ni uzembe au mtu anayefanya ana matatizo ya akili. Siwezi kuamini kati ya mtu ambaye hana mpangilio, kazi ambayo ni ya hovyo, duni na isiyoeleweka.

Somo; kuwa na mpangilio kwenye kila eneo la maisha yako, tenga muda wako kwa mambo sahihi na utumie hivyo, pangilia vizuri eneo lako la kazi na kila eneo la maisha yako pia. Usiwe mtu wa kukurupuka na kufanya kila kinachokuja mbele yako. Tenga muda wa kazi na fanya kazi, tenga muda wa kupumzika na pumzika. Kazi yako ifanye kwa namna ambayo mtu akiona anajua kweli umeweka juhudi kwenye kuifanya.

Nane; heshimu kazi yako.

Amelia; usijione wewe ni bora kuliko kazi au biashara yako. Kuwa mnyenyekevu, heshimu kile unachofanya na kipe heshima na umakini wa kutosha. Hata kama kuna vitu vingine unafanya, usichukulie kitu hicho kama ni cha pembeni. Kama ni mwandishi na pia ni daktari, usichukulie uandishi kama kitu cha pembeni, bali kipe heshima kama kitu kikuu kwako.

Somo; weka moyo wako wote, akili yako yote na umakini wako wote kwenye kile unachokifanya. Kwa maana hiyo, unahitaji kuchagua vitu vichache ambavyo utavifanya vizuri kwa kuweka kila kitu chako kwenye vitu hivyo na kupuuza vitu vingine vyote. Acha kuhangaika na kila kitu, kutawanya nguvu na umakini wako, maana hilo litakuzuia wewe kufanikiwa.

Tisa; usiwe na hasira.

Amelia; usiangukie kwenye hasira na hisia nyingine hasi pale unapokutana na majaribu. Mara zote kuwa na furaha na moyo mkunjufu, ifanye kazi yako kwa moyo mmoja na amua kuweka kila kikwazo pembeni. Na zaidi ya yote kuwa na furaha huku ukijua utapata unachotaka kama hutakata tamaa.

Somo; mambo hayatakwenda kama ulivyopanga, utakutana na vikwazo vya kila aina, wakati mwingine watu watakuzuia au kukukwamisha kwa makusudi kabisa. Hali hiyo itaibua hisia hasi ndani yako, hasira, chuki, kinyongo na nyingine. Epuka kuruhusu hisia hizo kukutawala, badala yake ziondoe na tawaliwa na hisia chanya ya furaha na matumaini. Endelea kuweka juhudi huku ukijua kila kikwazo kitashindwa kama wewe hutakata tamaa.

Angalizo; Amelia anatoa angalizo hili kuhusu siri hizi za mafanikio; kuna watu unaweza kuwaona wamefanikiwa kwa kutumia njia ambazo siyo sahihi, lakini jua hili, mafanikio yao hayatadumu kwa muda mrefu. Asili huwa haiibiwi, huwa inalipa kila ambacho mtu anafanya. Anayepata mafanikio kwa njia zisizo sahihi atalipa kwa kuyapotea. Na wewe unayetumia njia sahihi, hata kama utachelewa, utafikia mafanikio makubwa kama unavyotaka.

Amelia pia anashirikisha kwamba msingi wa mafanikio yake ulijengwa miaka mingi kabla hajafanikiwa. Alianza kuyaona mafanikio baada ya miaka 45 ya kazi bila ya kuchoka ndiyo alipata alichokitaka. Anasema mara nyingi akili yake ilikwamisha, mikono yake ilimkwamisha, miguu yake ilimkwamisha, lakini anashukuru roho yake haikuwahi kumwamisha.

Na hicho ndiyo unachohitaji ili ufanikiwe, roho ambayo haitakukwamisha, imani na matumaini kwamba licha ya kupitia magumu, bado utafanikiwa kama tu hutakata tamaa.

Rafiki yangu nikukaribishwe twende pamoja kwenye safari hii ya mafanikio, kwa kuwa ndani ya KISIMA CHA MAARIFA, kama bado hujawa mwanachama tuma ujumbe wenye maneno KISIMA CHA MAARIFA kwenda wasap namna 0717396253 na utapata maelekezo ya kujiunga na KISIMA CHA MAARIFA.

Rafiki, kama ungependa kuendelea kupokea makala na mafunzo mengine mazuri kwenye email yako, fungua hapa na ujaze fomu; www.bit.ly/amkaemail

Makala Hii Imeandikwa Na Dr. Makirita Amani Ambaye Ni Daktari Wa Binadamu, Kocha Wa Mafanikio, Mwandishi Na Mjasiriamali.

Kupata vitabu na uchambuzi wa kina wa vitabu jiunge na channel ya SOMA VITABU TANZANIA kwa kufungua kiungo hiki; www.t.me/somavitabutanzania