Tunapenda kupendwa, na hilo ndiyo linalotusukuma kwenye mambo mbalimbali tunayofanya.
Tunavaa nguo nzuri ili tupendwe, tunafanya yale wengine wanafanya hata kama hatutaki kuyafanya ili tu tupendwe.
Kuna wakati tunaenda mbali na hata kufanya mambo ambayo siyo sahihi kwetu, ili tu tupendwe.
Sasa leo nina ujumbe wa tofauti kwako rafiki yangu, hitaji lako la kupendwa kuwa ndiyo msukumo wako mkuu, linayaharibu maisha yako.
Unapokazana kufanya yale ambayo yatapelekea kila mtu akupende, unachagua kuishi maisha ambayo siyo yako, kitu ambacho hutakifurahia.
Kitu pekee unachohitaji kutoka kwa wengine ni wakuheshimu, wakishakuheshimu, wao wenyewe watakupenda bila hata ya wewe kuwalazimisha.
Hivyo kinachopaswa kukusukuma wewe siyo upendo, bali heshima, chochote unachofanya, usiangalie je watu watanipenda kwa kufanya hiki, bali jiulize je watu wataniheshimu kwa kufanya hivi.
Unapochagua kuyaishi maisha yako, siyo wote watakaokubaliana na wewe, wapo watakaokupinga na kukukosea, lakini wote watakuheshimu kwa maamuzi yako. Iwe mtu atakupenda au la, atakubaliana na wewe au la, mwisho wa siku atakuheshimu, kwa sababu anajua unasimamia nini.
Kupata heshima ya wengine, lazima kwanza wewe mwenyewe ujiheshimu, hakuna atakayeweza kukuheshimu kama wewe unajidharau. Kama unasema unasimamia kitu fulani, halafu kwenye matendo unakwenda kinyume na misimamo yako, hakuna atakayekuheshimu.
Eleza wazi ni wapi unasimama na kisha simama hapo, kama kuna mabadiliko yaeleze wazi na yasimamie, usifanye vitu kuwaridhisha wengine ili wakupende, bali fanya kile kinachokuridhisha na wengine watakuheshimu kupitia msimamo wako.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,
Ahsante sana kocha
Hii ni falsafa bora kuwa na jambo unalosimamia na wakikujua ili mradi ni sahihi watakuheshimu
Ni unafiki kufanya jambo kinyume kutafuta kupendwa kuficha baadh ya mambo kutafuta kukubalika ktk kikund cha watu
LikeLike
Karibu Hendry
LikeLike