#SheriaYaLeo (353/366); Kuwa na haraka na matamanio.
Unapokuwa na muda mwingi wa kufanya kitu, huwa inakuwa rahisi kuahirisha kufanya kitu hicho, kwa kujiambia utafanya kesho.
Tunapokuwa na muda mwingi huwa tunaishia kuupoteza kwa usumbufu na mambo yasiyokuwa na tija kwetu.
Inakuwa vigumu kuweka umakini wetu wote kwenye yaliyo muhimu na tunakosa hali ya uharaka.
Lakini pale muda unapokuwa umebaki mchache, tunakuwa na tahadhari kubwa. Tunautumia kwa mambo muhimu na hatuahirishi jambo, kwa kuwa tunajua hakuna muda mwingine.
Hivyo basi, swala la muda au kuahirisha linatokana na kuona upo mwingi.
Tunahitaji ukomo wa muda kutusukuma kuchukua hatua kwa haraka bila kuahirisha.
Uzuri ni kwamba ukomo huo wa muda tayari tunao muda wote.
Tunachohitaji ni kujikumbusha kuhusu kifo chetu.
Kwa kuwa hatutaishi milele na pia kwa kuwa hatujui kifo chetu ni lini, muda wetu ni mfupi sana.
Lakini tumekuwa tunajisahau kwa kuona muda tunao na hivyo kuishia kuupoteza na kuahirisha mambo.
Ili kuuthamini muda na kuwa kwenye hali ya uharaka bila ya kupoteza muda, tunapaswa kujikumbusha kuhusu kifo mara kwa mara.
Kila tunapoahirisha kufanya yaliyo muhimu, au kupoteza muda kwenye mambo yasiyo na tija, tunapaswa kujikumbusha jinsi muda wetu ulivyo mfupi na kifo kipo mbele yetu.
Kwa kujikumbusha kuhusu kifo na ufupi wa maisha yetu, tunaona jinsi ambavyo hatuna muda mwingi kama tunavyofikiria.
Hilo linatupa hali ya uharaka, kuweka umakini wetu kwenye yale muhimu na kutokuahirisha mambo.
Sheria ya leo; Tunapaswa kufikiria kifo chetu kama tarehe ya ukomo iliyo mbele yetu muda wote. Hilo linatukumbusha kutumia muda wetu vizuri na kwa tija badala ya kuupoteza na kuahirisha mambo.
#NidhamuUandilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji