Najua umeshasoma makala nyingi sana kuhusu mafanikio, makala ambazo zinasema mbinu hizi za mafanikio mbinu zile za mafanikio. Na unapoona makala nyingine tena inayokuambia kuna mambo kumi usiyoyajua kuhusu mafanikio, unaweza usiamini. Lakini twende pamoja na utagundua kwamba mambo haya kumi kuna ambayo huyajui kabisa na kuna ambayo unayajua ila uliyaelewa vibaya. Karibu twende pamoja na mwishoni utafanya maamuzi kama kweli unayataka mafanikio au unayatamani tu.
Katika mchezo wa riadha, au mbio, huwa tunapenda kuwaangalia wenzetu wakikimbia. Na katika mchezo huu kama wewe mwenyewe umewahi kushiriki au umekuwa unaufuatilia utakuwa unajua kwamba sio mbio zote ni sawa. Kuna mbio fupi na mbio ndefu, ambazo kwa jina jingine zinaitwa marathon.
Kama umekuwa ukiangalia wachezaji wa mchezo huu, jinsi wanavyoanza mbio fupi ni tofauti kabisa na jinsi wanavyoanza mbio ndefu. Kwenye mbio fupi wanaanza wakiwa na kasi ya juu kabisa kwa sababu wanajua ndani ya dakika moja mchezo umekwisha. Mwisho wao wanauona na hivyo wanakazana haraka iwezekanavyo wawe wa kwanza kufika. Kwa kweli ushindi kwenye mbio hizi fupi anapatikana haraka sana na anahitaji kuweza kutumia nguvu nyingi sana kwa wakati mfupi.
Kwa upande wa mbio ndefu, hapa mambo ni tofauti kabisa. Kwanza wachezaji wanaanza taratibu sana, wengine unaweza kufikiri wanatembea. Wanakwenda mdogo mdogo na kadiri muda unavyokwenda wanaendelea kuongeza mwendo. Mwisho wa mbio hizi hawauoni kwa haraka kwa sababu watazunguka sana mpaka kuja kufikia wanakotaka kuishia. Pia kwa mbio hizi mshindi anatokana na uvumilivu na kuweza kukazana kwa muda mrefu. Pia kama umekuwa unaangalia mbio hizi utaona wengi sana wamekuwa wanaishia njiani kwa kukata tamaa. Na pia umekuwa ukiona wale wanaoanza kwa kasi huwa wanakuja kupitwa na wale waliokuwa wanakwenda taratibu.
Maswali kutokana na huo mfano wetu wa leo;
1. Unafikiri mafanikio ni mbio fupi au ndefu?
2. Je ni kasi ipi unaendea nayo mafanikio?
3. Ni kipi kitakufanya usiishie njiani?
Tafadhali nitumie majibu ya maswali hayo kwenye email makirita@kisimachamaarifa.co.tz na kama unaisoma makala hii kwenye KISIMA CHA MAARIFA, weka majibu yako kwenye maoni hapo chini. Nitafurahi sana kusikia kutoka kwako.
Ni mambo yapi kumi ambayo siyafahamu kuhusu mafanikio?
1. Mafanikio ni mbio za muda mrefu.
Kama tulivyoona kwenye mchezo wa riadha, mafanikio sio mbio za muda mfupi na kama utayachukulia hivyo utapotea haraka sana. Mafanikio ni mbio za muda mrefu na hivyo sheria zote za mbio ndefu zinatumika hapa.
Anza kidogo na endelea kuongeza mwendo kadiri unavyokwenda, ni sheria muhimu sana ambayo watu wengi huwa hawaifanyii kazi. Usikurupuke na kuanza kufanya mambo kama dharura, chochote unachofanya, anza kidogo na endelea kuusoma mchezo kadiri unavyokwenda.
Mafanikio ni mbio ndefu, hutaona mwisho wa mbio zako. Ila unatakiwa ujue kwenye akili yako kwamba una safari ndefu ya kwenda na pia hutakiki kukata tamaa.
2. Mafanikio sio ajali.
Mafanikio hayatokei kwa mara moja kama inavyotokea ajali, hata ajali nayo ina visababisho vyake. Mafanikio yanatengenezwa na yanatengenezwa kwa muda mrefu sana. Mafanikio hayatokani na kitu unachofanya mara moja, hata kama kingekuwa kikubwa kiasi gani. Bali mafanikio yanatokana na vitu unavyofanya kila siku kwa kurudia rudia.
Mambo unayofanya leo yanaweza kuwa yanakusogeza karibu na mafanikio au yanakuondoa kabisa kwenye njia ya mafanikio. Ni vizuri sana ukazichunguza tabia zako za kila siku na ukajiuliza je hizi zinanipeleka kwenye mafanikio au zinanizuia kufikia mafanikio.
Ndio maana kwenye KISIMA CHA MAARIFA tuna kipengele cha tabia za mafanikio, kwa sababu kama hutajenga tabia bora za mafanikio, basi huwezi kufikia mafanikio. Hata ukipewa fedha nyingi utaishia kurudi pale ulipokuwa.
3. Mafanikio yanaanzia kwenye mawazo.
Kwa nini watu wengi wanakazana kufanya kazi kwa juhudi sana lakini hawapati mafanikio? Jibu ni rahisi sana, kwa sababu akili zao hazijaruhusu mafanikio. Kuna watu wengi sana ambao wamekuwa wakikimbiza mafanikio kwa mawazo wanayoweka kwenye akili zao wenyewe. Mtu anaweka juhudi lakini mawazo yake yote ni kwamba lazima atashindwa. Na unajua ni kitu gani kinachotokea? Anashindwa kama alivyojitabiria mwenyewe.
Akili yako ni mtumwa mzuri sana kwako ila ukishindwa kuiongoza inakufanya wewe kuwa mtumwa wake. Iongoze akili yako kwa kuweka mawazo chanya, mawazo kwamba unaweza, mawazo kwamba inawezekana na hatimaye utapata kile unachotaka.
4. Kuna wanaopenda mafanikio, kuna wanaotamani mafanikio na kuna waliojitoa kwa ajili ya mafanikio.
Kama hujajitoa kwa ajili ya mafanikio, hutayafikia na acha tu kupoteza muda wako. Tuna haja ya kujadili hayo mengine kweli? Maana unajua au kama hujui jua leo kwamba ili ufanikiwe ni lazima ujitoe, lazima ujikatae na ni lazima uwe tayari kufanya vitu ambavyo hupendi kufanya ili uweze kupata vitu ambavyo hujawahi kupata.
Ngoja tujadili hayo mengine kidogo ili uone ni wapi ambapo wewe unakwamba.
Kuna watu ambao wanatamani mafanikio, kila mtu anatamani maisha yake kuwa bora zaidi, kuweza kupata vitu anavyopendelea na kuonekana ni wa muhimu kwenye jamii inayomzunguka. Hakuna nguvu ya ziada unayohitaji ili kutamani, ila kama utaishia hapa kwenye kutamani, kila la kheri maana hata utamani kiasi gani mafanikio hayatakushukia.
Kuna watu ambao wanapenda mafanikio, angalau hawa wanafikiria ni jinsi gani ya kuyafikia, wanabadili hata mawazo yao na wanajaribu kufanya jitihada za kuyafikia. Hawa kidogo wanaweza kuyaonja mafanikio, ila hawayapati yale yenyewe kabisa.
Ni watu gani wanaopata mafanikio makubwa? Wale waliojitoa kwa ajili ya mafanikio. Hawa ni watu ambao hawakubali kurudishwa nyuma na kitu chochote kile. Wapo tayari kupambana mpaka wapate kile wanachotaka. Na unajua ni kitu gani kinatokea? Wanayapata mafanikio, maana unapokuwa mbishi, dunia inakuachia kile inachotaka, haitaki matatizo na wewe.
Jitoe.
5. Kuna kanuni ya mafanikio.
Watu wengi wamekuwa wakisema hakuna fomula ya maisha, kila mtu anabahati yake, kila mtu anaweza kutoka kivyake na maneno mengine mengi ya kijinga kama hayo.
Sasa leo naomba nikuambie kwamba kuna fomula ya maisha na kuna fomula ya mafanikio. Kama unabisha, una haki na maoni yako, endelea kubisha. Ila mimi pia ni mwanasayansi, na wanasayansi hatubishani kwa kelele bali kwa ushahidi. Na ushahidi unapatika kwa kufanya majaribio au utafiti.
Sasa naomba ufanye jaribio hili halafu uje na majibu; tafuta mafanikio unayotaka kwa njia yoyote ile unayotaka, haijalishi kama utaibia wengine au utawadhulumu, ishi maisha yoyote unayotaka, haijalishi kama ni mazuri kwako au kwa wengine. Usiwe na malengo yoyote, usihangaike kuamka kitandani, lala mpaka usingizi utakapoisha. Ukitaka furaha tafuta njia ya mkato ya kuipata, kunywa pombe, tumia madawa ya kulevya na utapata furaha ya muda, ikiisha ongeza tena. Halafu niambie utaishia wapi.
Maisha yana kanuni zake na mafanikio pia yana kanuni. Zijue na kuzifuata kanuni hizi na utafikia mafanikio. Zipuuze na utaendelea kujaribu kila siku bila ya kuyafikia.
6. Kanuni za mafanikio.
Kuna kanuni nyingi za mafanikio, kuna zile za asili ambazo zinatumika kwa watu wote na kuna zile za kila mtu ambazo unajiwekea mwenyewe.
Kanuni za asili za mafanikio ni;
A. Kufanya kazi kwa juhudi na maarifa. Hii ni namba moja popote pale, imeandikwa asiyefanya kazi na asile.
B. Kuwa mwaminifu. Kama huna uaminifu hakuna atakayekuamini, kama hakuna anayekuamini njia yako ya mafanikio imefika kikomo.
C. Kuwa mwadilifu. Fanya mambo yanayoendana na kile unachoamini. Ukaianza kujipinga wewe mwenyewe ni vigumu kufikia mafanikio.
D. Uvumilivu. Hakuna utakachofikia kwenye maisha kama huna uvumilivu. Maisha yana changamoto sana, sio rahisi kuzivuka.
E. Kujitoa. Tumeshajadili hapo juu.
Kanuni za kujitengenezea mwenyewe;
A. Malengo, kama huna malengo kwneye maisha yako utaishia wapi?
B. Imani, ni kipi hasa unachoamini.
C. Mtazamo chanya, hiki ni muhimu sana na unatakiwa kujitengenezea mwenyewe maana umezungukwa na wengi wasiokuwa nacho.
D. Ongeza nyingine…
E. Ongeza nyingine…
7. Mafanikio sio cheo kwamba utakufa nacho.
Ukisoma na ukapata cheo cha udaktari, wewe utaendelea kuitwa daktari mpaka utakapokufa, hata kama hutatibu mtu yeyote. Lakini mafanikio yako tofauti kabisa, ukifikia mafanikio leo, sio kinga kwamba utakufa na mafanikio hayo. Kesho unaweza kujikuta unaanzia chini kabisa. Hivyo ni muhimu sana kuendelea kufuata zile kanuni za mafanikio.
Watu wengi wamekuwa wakishindwa vibaya baada ya kufikia mafanikio kwa sababu wanaacha zile kanuni za mafanikio. Wanaona kwa vile wameshafanikiwa basi hawana haja ya kufuata tena zile kanuni. Loh wanajikuta wakiporomoka kwa kasi sana na inakuwa vigumu kwao kurudi tena pale walipokuwa.
8. Huwezi kufikia mafanikio kama hakuna anayekupinga.
Ni mara ngapi umekuwa ukipingana na maamuzi anayofanya mtu ambaye ana mafanikio? Mara nyingi mno. Hii ni kwa sababu jamii imekuwa inakudanganya kwamba unatakiwa uishi hivi unatakiwa uishi vile na wewe unafuata tu. Ni vigumu sana kufikia mafanikio, samahani, sio vigumu namaanisha huwezi kufikia mafanikio kama unafanya kile ambacho kila mtu anafanya. Acha kupoteza muda wako.
Ni lazima uende kinyume na matakwa ya wengi, ni lazima ufanye vitu ambavyo havijazoeleka, ni lazima watu wakupinge, wakukatishe tamaa, na ni lazima wewe ukatae yote hayo na kuendelea kujitoa mpaka utakapopata unachotaka.
9. Unaweza kufikia mafanikio kwa kufanya chochote unachopenda kufanya.
Kinacholeta mafanikio sio kile unachofanya ila jinsi unavyokifanya na kwa nini unakifanya. Kama unafanya kitu chochote kwa nia njema na kwa lengo la kufanya maisha ya wengine kuwa bora zaidi, tayari umeshafikia mafanikio, ni kuendelea tu kufanya ili uyafikie kwa ukamilifu.
10. Kujifunza kuhusu mafanikio na kutokufanyia kazi ni sawa na ambaye hajui kabisa.
Unaweza ukajifunza sana kuhusu mafanikio. Unaweza kusoma sana kuhusu watu waliofanikiwa, ila kama hutachukua hatua ni bora ya yule ambaye hajajifunza kabisa. Kama umesoma mambo haya kumi na unaondoka bila ya kubadili kitu chochote kwenye maisha yako, pole sana, utazunguka maisha kama mtu anayezunguka duara. Anaweza kutokwa jasho sana, ila amefika wapi? Amerudi pale pale.
Yatendee maisha yako haki kwa kufanyia kazi mambo yote unayojifunza na lazima utafikia mafanikio.
Mafanikio ni ya kila mtu ila hayatamshukia pale alipo. Ni lazima utoke na kwenda kuyatafuta mafanikio. Anza sasa kwa kufanyia kazi haya uliyojifunza.
Anza kwa kunipa majibu ya maswali tuliyoulizana pale juu, tushirikishe majibu yako kwenye maoni hapo chini. Na kama una jambo jingine la kutushirikisha usisite kuliweka hapo.
Mafanikio ni yako, yafanyie kazi.
TUPO PAMOJA.