Kwa asili yetu binadamu hatupendi kufanya vitu vigumu.
Na kama inatubidi kufanya basi huwa tunatafuta njia ya kurahisisha kufanya kitu hiko.
Hii ndio imeleta mapinduzi makubwa sana kwenye teknolojia ukianza na zama za mawe, zama za chuma, mapinduzi ya viwanda na mpaka sasa zama za taarifa.
Kwa kuwa vitu vingi vinaweza kurahisishwa, basi tunaamini kwamba kila kitu kinaweza kurahisishwa, kitu ambacho sio kweli na tunajinyima fursa kubwa sana.
Kuna kazi moja ngumu sana kwako kuifanya, lakini ni muhimu sana kuifanya. Na kama umechagua safari hii ya mafanikio, ni LAZIMA KUIFANYA.
Kazi hii ni kujijua wewe mwenyewe.
Kujijua wewe mwenyewe, kujijua hasa kwa undani, ni kazi iliyo ngumu kuliko kitu chochote ulichowahi kufanya. Na ni kazi muhimu sana kama unataka kuishi maisha bora, yenye furaha na mafanikio makubwa.
Ni lazima ujijue wewe mwenyewe vizuri ili uweze kujua kipi bora kwako.
Ni rahisi sana kuwajua wengine kuliko kujijua wewe binafsi.
Jamii inayotuzunguka inatulazimisha kuwa kama wengine walivyo, na hivyo tunakosa ile hamasa ya kutaka kujijua vizuri zaidi.
Tunaishi kwenye magereza mengi sana kwenye maisha yetu na magereza haya yanatokana na kutokujijua wewe mwenyewe. Magereza ya mahusiano, magereza ya kazi, magereza ya biashara na mengine mengi.
Unapojijua wewe mwenyewe unaweza kufanya maamuzi bora kwako na ukayasimamia.
Kama hujijui wewe mwenyewe utalazimika kufanya kile ambacho kila mtu anafanya. Na unapofanya kile ambacho kila mtu anafanya, ni vigumu sana, tena sana kuwa na maisha bora, ya furaha na yenye mafanikio.
Na cha kuumiza zaidi ni kwamba kazi hii huwezi kumlipa mtu akusaidie kuifanya, unahitaji kuifanya wewe mwenyewe. Hata ungekuwa na fedha nyingi kiasi gani, hata kama unasimamia majeshi makubwa, bado kazi hii unahitaji kuifanya wewe mwenyewe.
Na unaifanya kwa kupata muda wa kuwa na wewe mwenyewe, kutumia muda huu kuyatafakari maisha yako, kuangalia ni wapi umetoka, kuangalia ni vitu gani umekuwa unapendelea hasa na kuangalia ni vitu gani vinakupa hamasa kwenye maisha yako.
Hili sio zoezi la kufanya mara kwa mara, ni zoezi la kufanya kila siku. Ndio kila siku.
Anza sasa.
SOMA; Maswali matatu muhimu ya kujiuliza leo ili kujua muelekeo wa maisha yako.
TAMKO LANGU;
Kitu muhimu sana kwangu ni kujijua mimi mwenyewe. Najua ni kazi ngumu lakini nimechagua kuifanya kwa sababu nahitaji maisha bora, ya furaha na yenye mafanikio. Kila siku nitatenga muda wa kukaa na mimi mwenyewe ili kujijua vizuri. Nitaendelea kutafakari kuhusu maisha yangu na mimi mwenyewe kila siku.
NENO LA LEO.
Knowing others is wisdom, knowing yourself is Enlightenment.
Lao Tzu
Kuwajua wengine ni hekima, kujijua wewe mwenyewe ni ufunuo.
Jijue wewe mwenyewe, hii ni kazi muhimu sana kwako.
Rafiki na Kocha Wako,
Makirita Amani,
makirita@kisimachamaarifa.co.tz
TUPO PAMOJA.