Kila biashara ina msimu wake, nyingine zinaweza kuwa na msimu mrefu na nyingine zinaweza kuwa na msimu mfupi. Nyingine msimu ni miezi, nyingine msimu ni masaa.

Ni muhimu sana ujue msimu wa biashara yako. ujue ni wakati gani biashara inafanya vizuri, wateja ni wengi na ni wakati gani haifanyi vizuri na wateja sio wengi. Kwa kujua msimu wa biashara kutakuwezesha kujiandaa vyema wakati mzuri ili kuhakikisha unatengeneza faida nzuri. Na pia kujiandaa wakati ambao sio mzuri ili kuweka gharama za uendeshaji chini.

Kama hujui msimu wa biashara yako, unaweza kuona unapata faida sasa na kusahau kuna wakati mambo yatakuwa magumu. Hivyo ukafurahia faida na kutokujipanga kwa baadae, hali inayokuweka hatarini. Kwa sababu unapofika nyakati ngumu, biashara inashindwa kujiendesha yenyewe.

Hakuna biashara ambayo inaenda sawa kwenye wakati wote wa mwaka mzima, kuna wakati biashara itakuwa juu na kuna wakati itakwenda chini, kwa kuweza kujua nyakati hizi na kuzilinganisha vyema utaweza kuhesabu faida nzuri ya mwaka mzima. Badala ya kuhesabu miezi ya faida na miezi ya hasara.

Kwa mfano wakati biashara unafanya vizuri na hivyo faida ni kubwa hakikisha kwenye faida hiyo unatenga gharama zote za kuendesha biashara kwa mwaka mzima. Kwa hali hii hata miezi ambayo biashara haiendi vizuri, bado biashara itadumu kwa sababu ulishaandaa gharama za kuendesha biashara yako kwa kipindi kirefu.

Kujua msimu wa biashara yako ni muhimu sana, kama kweli unataka biashara hiyo idumu zaidi.

Kila la kheri kwenye biashara yako.

MUHIMU; Kama una swali, maoni au changamoto yoyote ya kibiashara, weka kwenye maoni hapo chini na tutajadiliana zaidi na kama itahitajika nitaandaa makala ya kuhusu jambo hilo kwenye makala zijazo.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz