Leo nataka nikupe siri kubwa sana kuhusu kila mtu unayekutana naye kwenye maisha yako. kwa kujua siri hii utakuwa umejiweka kwenye nafasi nzuri sana ya kuweza kufanya makubwa kwenye maisha yako.

Siri hii ni kwamba kila mtu unayekutana naye kwenye maisha yako, kuna vitu yeye anavijua ila wewe huvijui. Hii ni siri kubwa sana ambayo ukiweza kuitumia vizuri itakunufaisha sana.

Kila mtu, awe mkubwa au mdogo, awe amesoma au hajasoma, awe na kazi ya juu au ya chini, kuna kitu anakijua ambacho wewe hukijui, na kitu hiko ni muhimu sana kwa kazi yako, biashara yako au maisha yako kwa ujumla.

Kila mtu ametokea mazingira tofauti, malezi tofauti na amewahi kufanya mambo tofauti. Yote haya yanampa maarifa na uzoefu ambao wewe huna. Kupitia kile ambacho anajua mtu mwingine, unaweza kupata njia bora sana ya kuboresha kile unachofanya na maisha yako kwa ujumla.

Je unapata kile ambacho mtu anajua na wewe hujui?

1. Kwa kuwa mnyenyekevu, na kuwa tayari kujifunza. Kujua kwamba wewe hujui kila kitu na wengine pia wana mchango mkubwa katika kujifunza kwako.

2. Kwa kuwa tayari kusikiliza, kwa sababu hili ndiyo changamoto kubwa. Bila ya kusikiliza, hasa kusikiliza kwa makini, huwezi kupata kile ambacho wengine wanakijua.

3. Pia kwa kuuliza maswali, kuhoji zaidi. Unapopata nafasi ya kuwa na mtu, unaweza kumuuliza maswali kuhusu kile anachofanya, au maoni yake kulingana na kitu chochote kile ambacho utajifunza zaidi.

Kuwa tayari kujifunza kupitia wengi na utajifunza mengi sana ya kuboresha maisha yako.

SOMA; Hivi ndivyo TV na maoni ya wengine yanavyoharibu maisha yako, jihadhari sana.

TAMKO LANGU;

Nimejua ya kwamba kila mtu ninayekutana naye kwenye maisha yangu, kuna vitu anajua ambavyo mimi sivijui kabisa. Ni jukumu langu kuhakikisha najifunza kwa kila ninayekutana naye. Na nitaweza kujifunza kama nitakuwa mnyenyekevu, nitakuwa msikilizaji na kama nitahoji zaidi. Nipo tayari kujifunza kutoka kwa wengine, na nitajifunza mengi sana.

NENO LA LEO.

There is no end to education. It is not that you read a book, pass an examination, and finish with education. The whole of life, from the moment you are born to the moment you die, is a process of learning. – Jiddu Krishnamurti

Hakuna mwisho wa elimu. Siyo kwamba unasoma vitabu, kufaulu mtihani na kumaliza elimu. Maisha yako yote, tokea siku unayozaliwa mpaka siku unayokufa ni mchakato wa kujifunza, kila siku.

Rafiki na Kocha Wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz

TUPO PAMOJA.