Ni kuweka matarajio yako juu ya kitu chochote kile.

Unapoweka matarajio fulani kwenye kitu chochote unachofanya, kwa hakika lazima utapoteza.

Kwa sababu kama utapata kile ulichotarajia, ulishakitarajia tayari, hivyo hutakuwa na msukumo wa kukifurahia.

Na kama hutapata kile ambacho ulitarajia, utaumia zaidi kwa sababu hujapata ulichotarajia, utakasirika, kujidharau na hata kuona aibu kwamba hujapata ulichotarajia.

Njia pekee ya kuwa na maisha tulivu na unayoyafurahia, ni kutokuweka matarajio yoyote.

Hii haimaanishi uwe mzembe kwenye maisha, usiwe na malengo yoyote na ufanye chochote unachojisikia.

Badala yake inamaanisha ujue ni nini hasa unataka kwenye maisha yako, nini unapaswa kufanya ili kukipata, kisha kuweka juhudi zako zote katika kufanya kitu hicho, bila ya kuwa na matarajio yoyote.

Wewe kazana kufanya kwa uwezo wako wote, weka kila kitu kwenye juhudi unazofanya, kisha kuwa tayari kupokea matokeo yoyote utakayoyapata.

Yakija matokeo mazuri yafurahie na kazana kufanya kwa ubora zaidi. Yakija matokeo mabaya jifunze na usirudie tena kile kilicholeta matokeo hayo.

Lakini ukishaweka matarajio fulani, kwamba kwa kuwa umechukua hatua sahihi basi lazima upate matokeo uliyopanga, unajiandaa kuumia. Kwa sababu ukipata kama unavyotarajia utachukulia kawaida. Na ukikosa utajiumiza zaidi.

Maisha bila ya matarajio, maisha ya kuweka juhudi kwenye kile unachofanya na kuwa tayari kupokea matokeo yoyote ndiyo maisha yenye utulivu na furaha. Ishi maisha hayo.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Dr. Makirita Amani,

www.amkamtanzania.com/kocha