2296; Ukiweka Sifa Pembeni, Utafanya Makubwa.
Sisi kama binadamu tunasukumwa sana na sifa katika mengi tunayofanya.
Tunapojua kuna fursa ya wengine kutukubali na kutusifia kwa kile tunachofanya, tunasukumwa zaidi kukifanya.
Lakini ubaya wa kufanya kwa sifa ni unaweza kujikuta unafanya hata yasiyokuwa na manufaa kwa sababu tu unataka sifa.
Ipo kauli kwamba kila sifa, iwe nzuri au mbaya inamsaada kwa mtu.
Lakini hilo limeleta uharibifu kwa wengi.
Wengi wanaihangaika na kiki, zinawapoteza zaidi kuliko kuwasaidia.
Hivyo wewe weka sifa pembeni, sahau kabisa watu wanakuchukuliaje kwenye kile unachofanya na badala yake fanya kile kilicho sahihi.
Jipe wajibu wa kufanya kitu chenye manufaa kwa wengine, kitu kinachowasaidia, kitu kinachoongeza thamani zaidi kwenye maisha yao.
Kama kila wakati utakuwa unatafuta fursa za kufanya yaliyo sahihi, iwe watu wanaona au hawaoni, wanakisifia au hawakusifii, mara zote utafanya kulicho sahihi.
Wacha wengine wakimbizane na sifa, wewe kimbizana na kuwa wa manufaa, kuongeza thamani kwa wengine.
Na hilo hata halitakupa umaarufu, litakufanya ujisikie vizuri.
Na kujisikia huko vizuri hakuna mwisho, kwani una nafasi zaidi za kufanya yaliyo sahihi na yaliyo na manufaa kwa wengine.
Weka sifa pembeni na mara zote fanya kilicho sahihi, ambacho ni kile kinachowasaidia wengine na kuwafanya kuwa bora zaidi.
Kocha.