2916; Saa Mbovu.

Kwako rafiki yangu mpendwa unayetafuta kitu sahihi kabisa na chenye uhakika wa asilimia 100 ndiyo ukomae nacho.

Ukweli ni utasubiri sana nahuenda hutafanya chochote kabisa.
Hakuna kitu chochote ambacho kiko sahihi zaidi ya vingine vyote.
Kila kitu kina mazuri na mabaya yake, urahisi na changamoto zake.

Kadhalika hakuna kitu chochote ambacho kina uhakika wa asilimia 100. Kila kitu kina kiwango fulani cha hatari ndani yake. Kinachotofautisha ni kiwango cha hatari.

Unachohitaji ili kufanikiwa siyo kuwa na kilicho sahihi kuliko vyote, au kupata chenye uhakika wa asilimia 100.
Bali unachohitaji ni kuamua kwenye kitu kimoja kisha kuacha kuhangaika na vingine vyote.
Hata unapokutana na magumu, usiache, wewe endelea.
Hata unapoona kuna mengine rahisi na ya uhakika zaidi, usivunje maamuzi uliyofanya.

Kuelewa vizuri dhana hii, iangalie saa mbovu ya mshale. Saa itakuwa imesimama kabisa na haibadiliki. Kila utakapoiangalia itakuwa inasema majira ya uongo. Lakini mara mbili kila siku, mchana na usiku saa hiyo itakuwa sahihi.

Hiyo ndiyo nguvu ya kukomaa na kitu kimoja, utakosea sana, lakini kuna wakati utapatia na unapopatia ndipo kuna manufaa makubwa.

Watu wanahangaika na kila kitu kipya kinachokuja kwa kuona ni sahihi zaidi, rahisi zaidi au uhakika zaidi.
Wewe usidanganyike, hakuna kitu cha aina hiyo.
Kila kitu kina changamoto zake.
Utakianza kwa matamanio makubwa, lakini haitachukua muda utakutana na ugumu au changamoto zake.
Na hapo tena utaona kingine kizuri kufanya.

Huna muda wala nguvu za kupoteza kwenye kila kitu.
Fanya maamuzi ya nini unafanya.
Kisha komaa na maamuzi hayo kama saa mbovu.
Ndiyo utakosea.
Lakini kumbuka saa mbovu.
Kuna wakati utapatia.
Na huo ndiyo wakati pekee muhimu.

#NidhamuUandilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#BilioneaMafunzoni
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe