3306; Kukubali kuwa kawaida.

Rafiki yangu mpendwa,

Watu wengi wamekuwa kawaida kwenye maeneo yote ya maisha yao, kitu ambacho kinawafanya wasipate mafanikio makubwa ambayo wangeweza kuyapata.

Kinachosababisha hilo ni wao kutaka kufanya kila kitu, kudhani wanaweza kuwa bora kwenye vitu vyote.
Hapo wanagawa rasilimali zao kwa usawa kwenye mambo mengi wanayofanya.

Matokeo yake yanakuwa ni kuwa kawaida au hata chini ya kawaida kwenye mambo hayo mengi.

Kupata mafanikio makubwa, unapaswa kwenda kinyume na hayo.
Kwanza kabisa unapaswa kuchagua eneo moja pekee ambalo ndiyo utakwenda kuweka rasilimali zako zote ili kuwa bora kabisa.
Halafu unakubali kuwa kawaida kwenye maeneo mengine yote.

Hapo unakuwa umechagua kuwa bora sana kwenye eneo hilo moja na kawaida kwenye maeneo mengine.
Eneo hilo ndiyo unalipa umakini wako wote na kuhakikisha pale watu wanapoongelea mtu aliye bora kwenye hilo, jina la kwanza kufikiria liwe lako.

Ukitaka kuwa bora kwenye kila kitu, unapunguza nguvu yako ambayo ungeweza kuitumia vizuri kubobea kwenye eneo moja.

Kuondokana na hilo la kujaribu kuwa bora kwenye kila eneo, lazima uanze kwa kukubali unaenda kuwa kawaida kwenye hayo maeneo.
Maamuzi hayo yatakupa uhuru wa kupeleka umakini wako wote kwenye eneo moja ulilochagua bila ya kuona unapoteza fursa za kila mahali.

Unaona jinsi mambo yanavyokuwa kinyume hapo, ukitaka kuwa bora kwenye maeneo yote, unaishia kuwa kawaida kwenye yote.
Lakini ukichagua eneo moja unalotaka kuwa bora zaidi na kukubali kuwa kawaida kwenye maeneo mengine, unapata mafanikio makubwa zaidi.

Kufokasi na ung’ang’anizi vinahitajika sana. Kwani ukishachagua eneo moja unalotaka kuwa bora, haimaanishi mambo yatakuwa rahisi. Utakutana na vikwazo vingi, hupaswi kuona kama ndiyo mwisho na kwenda kwenye mambo mengine.
Unapaswa kuendelea na kile ulichochagua mpaka upate matokeo ambayo ulipanga kupata.
Usikubali chochote ambacho ni chini ya kile hasa unachotaka kufikia.

Kwa nini wengi hawafanyi jambo hili linaloonekana kuwa rahisi kabisa kwenye kujenga mafanikio makubwa?
Jibu ni watu kutokukubali kuwa kawaida kwenye maeneo mengine mengi.
Wengi hudhani wanaweza kuwa bora kwenye maeneo mengi, hivyo wanahangaika nayo kwa pamoja, kitu kinachopelekea wawe kawaida kwenye maeneo yote.

Kuweka pembeni mambo ambayo tayari yanakupa majibu ili kuwa bora kwenye eneo moja ni kitu kinachohitaji utulivu wa hali ya juu na mtu kujiamini na kujikubali.
Hayo yatakufanya uweze kuweka kila ulichonacho ili kufanikiwa kwenye hayo machache.

Chagua kuwa bora kwenye eneo moja na kawaida kwenye maeneo mengine, la sivyo utaishia kuwa kawaida kwenye mambo yako yote.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe