Makosa ya wengine ni kitu cha kipekee sana kwetu,

Makosa ya wengine yanaonekana haraka sana, kuliko hata makosa yetu.

Makosa ya wengine yanatupa vitu vya kujadili na kukosoa.

Makosa ya wengine yanatupa ahueni kwamba angalau sisi tuko vizuri, kuliko hao wenye makosa hayo.

Makosa ya wengine tunaweza kuamua kuyatumia tutakavyo, kwa faida zetu binafsi.

Tunapenda kuongelea makosa ya wengine kuliko ya kwetu, lakini hili halifanyi makosa yetu kuwa madogo kuliko ya wengine. Na wala halipunguzi makosa yetu sisi.

Acha sasa kutumia sana makosa ya wengine kwa faida zako binafsi. weka nguvu zako kwenye makosa yako. angalia ni yapi umeshindwa kufanya au umefanya kwa makosa. Na kisha fanya marekebisho.

Kama kuna makosa unaona wengine wamefanya, unaweza kujifunza kupitia makosa hayo, lakini siyo kuyatumia kwa njia nyingine yoyote. Na kama unaweza kuwa msaada kwa wale waliofanya makosa, fanya hivyo.

Njia nyingine yoyote utakayoitumia kwa makosa ya wengine ni njia batili, haitakusaidia wewe wala yule aliyefanya makosa. Badala yake itakuwa na madhara hasi, kwako unayeongelea makosa hayo utasahau yako, na kwa yule unayemwongelea makosa yake ataogopa hata kujaribu kufanya mambo makubwa, au kukata tamaa.

SOMA; SIRI YA 16 YA MAFANIKIO; Jifunze Kutokana Na Makosa Yako Na Jipange Kufanikiwa.

TAMKO LANGU;

Nimejua ya kwamba ni rahisi sana kufuatilia na kujadili makosa ya wengine kuliko makosa yangu binafsi. lakini kujadili makosa hayo hakuna msaada wowote kwangu au kwa mwenye makosa. Kuanzia sasa nitaacha kutumia makosa ya wengine kwa faida zangu binafsi. badala yake nitajifunza kupitia makosa haya na kuwasaidia pale ninapoweza.

NENO LA LEO.

“Freedom is not worth having if it does not include the freedom to make mistakes.” ― Mahatma Gandhi

Hakuna maana ya kuwa na uhuru kama uhuru huo haukupi nafasi ya kufanya makosa.

Kufanya makosa ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Usikazane kuangalia tu makosa ya wengine, angalia makosa yako na yafanyie kazi.

Rafiki na Kocha Wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz

TUPO PAMOJA.