Kama umekuwa msomaji wa makala hizi za KURASA ZA MAISHA YA MAFANIKIO, mpaka sasa utakuwa umeshagundua kitu kimoja kikubwa, kwamba msingi wa kila kitu tunachofanya kwenye maisha yetu ni UAMINIFU. Watu watafanya biashara na wewe kutokana na uaminifu wako. Watu watakuajiri na kuendelea kuwa na wewe kwa sababu ya uaminifu. Familia yako itakuwa imara na mahusiano yako yatakuwa bora kwa sababu ya uaminifu.
Kama kuna kitu kimoja tunachopaswa kukilinda sana kwenye maisha yetu basi ni uaminifu, kwa sababu bila ya uaminifu hakuna kikubwa tunachoweza kufanya kwenye maisha yetu. Tunaweza kuponzwa na manufaa ya muda mfupi, na tukaharibu uaminifu wetu na kujizuia kupata manufaa makubwa zaidi baadaye.
Sasa swali linakuja, ni njia ipi bora ya kuwa mwaminifu? Na kwa sababu watu wanapenda SIRI, wanaweza kuuliza zipi siri za kuwa mwaminifu? Na majibu ni kwamba hakuna siri kubwa, njia bora ya kuwa mwaminifu ni moja tu; KUWA MWAMINIFU.
Utakuwa mwaminifu kwa kuwa mwaminifu. Huhitaji darasa wala mwongozo wa kuwa mwaminifu, unachohitaji ni kuanza kuwa mwaminifu, sasa hivi, leo hii. Anza na vitu vidogo vidogo, unavyojiahidi mwenyewe na uvitimize. Kwa njia hii uaminifu wako unaanza kukua na unajikuta ukiweza kusimamia mambo makubwa yanayowashinda watu wengi.
Unapokuwa mwaminifu huangalii nani anaona au haoni, unakuwa mwaminifu kwa sababu umeamua kuwa mwaminifu na wala siyo kwa sababu unataka uonekane hivyo. Hii ni changamoto kubwa kwa sababu wengi wamekuwa wakifanya mambo ya uaminifu mbele ya wengine, lakini wanapokuwa wenyewe, au wanapokuwa pale ambapo hakuna wale ambao wanataka kuonesha uaminifu kwao, wanafanya mambo ambayo siyo ya uaminifu.
Kwa kufanya hivi wanajiharibia wao wenyewe, wanajidanganya wao wenyewe. Wanafikiri wanaidanganya dunia, lakini dunia ni janja kuliko mtu yeyote yule, unaweza kujidanganya tu mwenyewe, huwezi kuidanganya dunia. Kwa sababu hata ufiche kiasi gani, kuna siku kila kitu kitakuwa hadharani. Na siku hiyo siyo mbali. Usitake kuwa na maisha ya sura mbili, kwa sababu muda siyo mrefu sura zote zitaonekana na ile mbaya ndiyo itakayochukuliwa.
Hakuna maisha rahisi kama maisha ya uaminifu, maisha ambayo hukazani kutengeneza hadithi mbalimbali zitakazoendana na watu mbalimbali, maisha ambayo huhitaji kujikumbusha ulidanganya nini ili usijikanyage.
Njia bora ya kuwa mwaminifu ni kuwa mwaminifu, kwenye kila kitu unachofanya kwenye maisha yako, iwe uko mwenyewe au uko mbele ya wengine. Fanya kile ambacho uko tayari kujivunia, kile ambacho utafurahia kama kitachapishwa kwenye kurasa za mbele za magazeti yote na kuoneshwa moja kwa moja kwenye televisheni zote.
Kuwa mwaminifu kwa kuwa mwaminifu, ni maisha rahisi na bora sana kuchagua kuishi.
TUPO PAMOJA.
KOCHA MAKIRITA.
SOMA; UKURASA WA 51; Uadilifu, Kioungo Muhimu Cha Kufikia Mafanikio.