Watu wengi wakisikia umasikini, moja kwa moja wanakwenda kwenye fedha. Kwamba masikini ni yule ambaye hana fedha za kutosha. Lakini umasikini upo kwenye kila eneo la maisha yetu, na yapo maeneo ambayo tunahitaji kuwa makini zaidi kwa sababu umasikini wake una madhara makubwa kwetu.

IMG-20170314-WA0002

Moja ya maeneo hayo ni muda. Umasikini wa muda ni kitu kinachowazuia wengi kufanikiwa. Hii ni kwa sababu muda ni ule ule kila siku, lakini mambo ya kufanya yanazidi kuwa mengi kila siku. Hakuna anayeweza kuongeza muda wake na hivyo juhudi za kuondoa umasikini huu lazima ziwe tofauti sana na zile za kuondoa umasikini wa fedha.

Kama huna fedha unafanya kazi kupata fedha zaidi, hakuna kikomo cha fedha unazoweza kupata bali kile unachojiwekea mwenyewe. Lakini kwenye muda unahitaji mbinu tofauti ili usiwe na kikomo cha muda.

Katika kuondokana na umasikini wa muda, kitu muhimu unapaswa kujua ni hichi; huna muda wa kuweza kufanya kila kitu, ila una muda wa kuweza kufanya yale ambayo ni muhimu zaidi.

Hivyo unapoanza na muda, anza na vipaumbele, anza na yale ambayo ni muhimu zaidi, ambayo hayawezi kufanyika kama wewe haupo. Haya ndiyo yanapaswa kuchukua muda wako na mengine yote weka pembeni.

SOMA; Chanzo Kikuu Cha Umasikini Au Utajiri.

Hatua nyingine muhimu, kwa kuwa umeshaondokana na yale ambayo siyo muhimu, lakini lazima yafanywe. Hivyo unahitaji watu watakaokusaidia kufanya yale ambayo siyo yalima uyafanye wewe mwenyewe. Unaongeza muda wako zaidi kwa kuwa na watu wanakusaidia kwa yale ambayo unahitaji kuyafanya lakini hayafikii kipaumbele cha muda wako.

Unaweza kuongeza muda wako maradufu kulingana na idadi ya watu wanaokusaidia yale majukumu ambayo ilibidi ufanye wewe mwenyewe. Ukiwa na watu kumi wanaokusaidia kazi zako kwa masaa 8 kwa siku, ina maana kwa siku umepata masaa 80 ya ziada.

Vipo vingine vingi vya kufanya kwenye kupambana na umasikini wa muda, kama kusema hapana, kuacha kufuatilia mambo ya wengine, kuacha kulalamika na kulaumu na kudhibiti matumizi yako ya mitandao na kufuatilia habari.

Vita yako kuu, kadiri unavyozidi kufanikiwa ni umasikini wa muda. Kadiri unavyofanikiwa zaidi ndivyo unavyozidi kuwa na umasikini wa muda. Ndiyo maana unahitaji kuweka juhudi za dhati kuepuka umasikini huu.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa ushauri na Coaching bonyeza maandishi haya kupata utaratibu.

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea MOBILE UNIVERSITY (bonyeza hayo maandishi.)

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea MTAALAMU NETWORK