Mwanafalsafa Seneca anatukumbusha kwamba kila siku tunahitaji kupata muda wa kutafakari kuhusu maisha yetu na kile tulichofanya siku nzima.
Mwisho wa siku, tunahitaji kupata muda wa kujiuliza siku yetu imekwendaje na yale tuliyofanya tumefanyaje.
Ni yapi ambayo tumefanya vizuri,
Yapi ambayo tumekosea na
Yapi ambayo tunaweza kuboresha zaidi.
Epictetus yeye anakwenda mbali zaidi na kutuambia tunapaswa kuishi siku yetu kama washiriki na kama watazamaji. Tunakuwa washiriki kwa yale tunayofanya na tunakuwa watazamaji kwa kuangalia ni namna gani tumeishi misingi ya ustoa.
Marcus Aurelius yeye kila siku alikuwa akiandika kwenye kijitabu chake namna siku hiyo ilivyokwenda na yale aliyojifunza.
Mwisho kabisa, falsafanya ustoa ni falsafa ya matendo na siyo maneno pekee. Hivyo kujipima kama kweli unaiishi, unapaswa kuangalia matendo yako na namna ambavyo unachukulia yale yanayotokea.
Kwa mfano kama umeenda kwenye sherehe, na uliamini unaheshimika na hivyo kutarajia kupangwa viti vya mbele, lakini ukajikuta umepangwa viti vya nyuma. Hapa unaweza kuona umedharauliwa na hata kuwaonea wivu wale waliokaa mbele, lakini kama mstoa, unapaswa kujiuliza, kuna tofauti gani kuuweka mwili wako kiti cha mbele na kiti cha nyuma? Utagundua hayo yote hayapaswi kukusumbua.
Kujua kama unaishi ustoa na kama una faida kwako, jiangalie namna unavyodhibiti tamaa zako, unavyochukulia mambo ma hata unavyoishi maisha yako, badala ya kusema, unafanya.