Habari za asubuhi ya leo rafiki yangu?
Hongera kwa siku hii nyingine nzuri sana ya leo, nafasi ya kipekee kwetu kwenda kuweka juhudi kubwa ili kuweza kupata matokeo bora kabisa.
Msingi wetu wa maisha ya mafanikio ni NIDHAMU, UADILIFU na KUJITUMA ambapo tunakwenda kufanya makubwa leo na kila siku ya maisha yetu.
Asubuhi ya leo tutafakari kuhusu KAZI NI NZURI…
Watu wengi wanaposikia neno kazi, wanajisikia vibaya,
Wanaona kama ni sehemu ya kuteseka,
Sehemu ambayo wanachagua kuumia siku tano za wiki, ili waweze kupumzika na kufurahia siku mbili za mwisho wa wiki.
Lakini kinacholeta yote hayo ni mtazamo wetu juu ya kazi.
Tunapokuwa na mtazamo kwamba kazi ni mbaya na ni njia ya kuteseka, hicho ndiyo tunapata.
Lakini tunapokuwa na mtazamo sahihi juu ya kazi,
Kwa kuamini kazi ni nzuri, tunapenda kile tunachofanya na kuweza kufanikiwa.
Kazi ni nzuri, siyo tu kwa sababu unataka kujenga mtazamo chanya, bali kuna kila aina ya ushahidi kwamba kazi ni nzuri.
Kazi ni nzuri kwa sababu inatuwezesha kufanya maisha ya wengine kuwa bora zaidi.
Kazi ni nzuri kwa sababu inatuwezesha kutengeneza kipato cha kuendesha maisha yetu.
Kazi ni nzuri kwa sababu inatuletea uhuru wa namna gani tuendeshe maisha yetu.
Kazi ni nzuri kwa sababu inatuletea furaha, pale tunapoona tunachowapa wengine.
Kwa vyovyote vile kazi ni nzuri na ikifanywa vizuri inayafanya maisha kuwa mazuri pia.
Futa kila mtazamo hasi ulioweka kwenye akili yako kuhusiana na kazi. Weka mtazamo huu mkuu kwamba kazi ni nzuri kisha ipende kazi yoyote ile ambayo unaifanya.
Nakutakia siku njema sana ya leo, uende ukafanye makubwa na kuweza kupata matokeo bora.
Rafiki yako,
Kocha Makirita Amani,
MAFANIKIO NI HAKI YAKO YA KUZALIWA.