Kila mmoja wetu anapenda kuwa na maisha yenye uhuru, kuweza kufanya kile anachotaka kwa wakati anaotaka.
Lakini wengi pamoja na kuweza kupata uhuru wao kutoka kwa wengine, yaani kutowajibika chini ya wengine, bado wanakosa uhuru wao kutoka kwa wao wenyewe.
Watu hawa wanakuwa watumwa wa nafsi zao wenyewe, na kujikuta hawana ule uhuru waliokuwa wanautaka kwenye maisha yao, na pia wanashindwa kujiondoa kwenye utumwa waliojiweka.
Utumwa mkubwa ambao watu wanajijengea wenyewe ni kushikamana na vitu au watu fulani kwenye maisha yao.
Kushikamana na vitu, ni pale ambapo mtu unajiambia kwamba maisha yako hayawezi kwenda kama hujapata kitu fulani unachotaka. Na kushikamana na watu ni pale unapojiambia maisha yako hayawezi kwenda bila ya kuwa na watu fulani ambao tayari umeshawazoea.
Ni kweli kwenye maisha unahitaji kuwategemea wengine na pia unategemea vitu mbalimbali ili maisha yako yaweze kwenda, lakini ukishafikia hatua ya kujiambia maisha yako hayawezi kwenda kama utakosa vitu fulani au kama utawakosa watu fulani, jua huna tena maisha hapo, bali upo kwenye utumwa.
Upo huru kwa kiwango ambacho unaweza kuachana na kitu au mtu yeyote mara moja na maisha yako yakaendelea vizuri, bila ya shida yoyote.
Upo huru kwa kiwango ambacho unaweza kusimama hata baada ya kuanguka au kuangushwa na vile vitu ambavyo ulivitegemea sana.
Kushikamana na vitu au watu kunakuja kwa namna hii;
Pale mtu anapofanya kitu ambacho hukutegemea afaye, halafu wewe ukachukia sana na hata kuharibu mipango yako mingine, hapo umeshikamana na kutaka watu wawe kama unavyotaka wewe, kitu ambacho ni kigumu sana kwako kufanikisha.
Kama unajiambia huwezi kulala bila ya kula au kunywa kitu fulani au siku yako haiwezi kwenda bila ya kupata kitu fulani, umeshikamana na kitu hicho na utakuwa mtumwa wako mwenyewe.
Chochote unachokimbilia kufanya na kujiona huwezi kuacha kufanya, hata kama hakina umuhimu mkubwa kwako ni kushikamana na kitu hicho na kupoteza uhuru wako.
Kila tatizo kwenye maisha yako linatokana na kushikamana na vitu ambavyo vipo nje ya uwezo wako. Kila unachokazana nacho ni kwa sababu umeshikamana nacho.
Ili kufikia uhuru kamili na kuondokana na utumwa huu wa ndani yako binafsi, unahitaji kutengeneza akili ambayo haishikamani na chochote.
Akili ambayo haitegemei vitu viende kwa namna unavyotaka wewe, haitegemei watu wawe na tabia fulani ndiyo ufurahi. Unahitaji kutengeneza akili ambayo ipo tayari kwa chochote na inachukua kila kinachokuja na kukitumia.
Ili kutengeneza akili ambayo haishikamani na chochote, unapaswa kujifunza na kufanyia kazi kuachilia. Kuwa tayari kuachilia chochote na yeyote.
Achilia kwa kuruhusu ndani ya akili yako watu wawe kama wanavyotaka kuwa na vitu viende kama vinavyotaka kuenda. Usilazimishe kila kitu kiende kama unavyotaka wewe, kwa sababu hilo lipo nje ya uwezo wako. Achilia na utajijengea uhuru mkubwa sana kwako.
Pia acha ubinafsi, acha kuona kama dunia inapaswa kukupa wewe kila unachotaka na kwa wakati ambao unataka. Acha kulazimisha kila kitu kiende kwa matakwa yako. Hilo lipo nje ya uwezo wako na kadiri unavyoshikamana nalo ndiyo unavyozidi kukosa uhuru.
Mwisho kabisa, kuza mtazamo wako zaidi, anza kuangalia mitazamo ya wengine pia na siyo kujiangalia wewe mwenyewe tu. Ona jinsi wengine wanavyoshikamana na vitu na kuteseka, na jua kila mmoja wetu kuna namna anateseka na kushikamana na vitu. Kwa kuwa na mtazamo wa aina hii, itakusaidia kujijenga uhuru wako na kuacha kushikamana na vitu.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,