Kuna vitu vingi sana huwa tunavyo, tunakuwa tumevizoea na kuvichukulia kawaida sana, kwa sababu tumeshakuwa navyo kwa muda na tunajua tutaendelea kuwa navyo.
Kwa kuzoea kwetu vitu hivyo, huwa tunaona havina thamani kubwa sana kwetu, na tunaweza kuviacha hovyo hovyo na kusahau kabisa kwamba mwanzoni tuliteseka sana kuvipata.
Pale inapotokea tunakosa vitu hivyo tulivyovizoea, ndiyo sasa tunaona umuhimu wake mkubwa, ndiyo tunaona namna gani vina thamani kubwa kwetu, ndiyo tunajifunza kwamba maisha yetu yanakuwa magumu sana bila ya kuwa na vitu hivyo.
Kwa kifupi, wengi huwa tunaona thamani na umuhimu wa vitu baada ya kuwa tumevipoteza. Pale tunapogundua kwamba hatuwezi kuwa tena na vitu hivyo, ndipo tunajuta kwa nini hatukuvipa umuhimu mkubwa wakati tulipokuwa navyo.
Rafiki, chochote ulichonacho sasa, usikichukulie poa hata kidogo, usilete mazoea kwenye chochote ulichonacho, kithamini sana kwa sababu ulisumbuka kukipata. Pia kijali sana kwa sasa kwa sababu kitakapoondoka utakikosa sana.
Hakuna chochote ulichonacho sasa ambacho hukusumbuka kukipata, usikubali udhaifu wetu binadamu wa kuzoea vitu ukufanye ushindwe kuthamini vile vitu ambavyo umekaa navyo kwa muda mrefu.
Kila kitu kina thamani na umuhimu mkubwa kwako, chagua kuelewa thamani hii kila siku kabla hujaja kujuta pale unapopoteza kitu ambacho ulikuwa umekizoea na hukuwa unakithamini.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,