Tunapokuwa na mambo mengi ya kufanya huku muda wetu ukiwa mfupi, huwa tunapata msongo wa mawazo. Huwa tunafikiri kinachotupa msongo ni yale mambo mengi tuliyonayo ya kufanya, lakini hilo siyo sahihi.

Kinachotupa msongo siyo yale mambo mengi tuliyonayo ya kufanya, bali namna tunavyofikiri kuhusu mambo hayo.

Kinachotupa msongo wa mawazo ni kushindwa kudhibiti fikra zetu kwenye yale mambo mengi ambayo inabidi tuyafanye.

Kwa kuwa tuna mambo mengi ya kufanya, na labda muda siyo rafiki kwetu, wakati tunafanya jambo moja, tunafikiria jambo jingine ambalo hatujafanya. Hali hii ndiyo inayotufanya tuwe na msongo.

Kama tukiweza kuzidhibiti fikra zetu na kuziweka kwenye lile tunalofanya kwa wakati huo na kutokuyumbishwa na yale mengine ambayo yanatusubiri kufanya, msongo wa mawazo utaondoka kabisa.

Tunachohitaji kufanya ni kimoja tu, weka fikra zako kwenye kile unachofanya kwa wakati huo na achana na mengine yote. Hata kama yale mengine ni magumu na muhimu kiasi gani, haitakusaidia kuyafikiria wakati una kitu kingine cha kufanya.

Jipe uhuru wa kuweka fikra zako kwenye kile unachofanya kwa wakati huo na linapokuja wazo kuhusu kingine unachopaswa kufanya liandike mahali na achana nalo. Wakati wa kufanya jambo hilo ukifika utaweza kulifikiria kwa namna utakavyo.

Usiharibu ufanyaji wa jambo moja kwa sababu unafikiria mambo mengine, weka fikra zako kwenye kila unachofanya na utasahau kuhusu msongo wa mawazo.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Dr. Makirita Amani,

www.amkamtanzania.com/kocha