Hakuna kitu ambacho sisi binadamu tunakiogopa kama kukaa bila ya kufanya kitu. Tumejizoesha kwamba kila wakati lazima tuwe na kitu cha kufanya, la sivyo hatujawa makini na maisha yetu.
Hakuna ubaya wowote kuwa na kitu cha kufanya kila wakati, lakini ni hatari sana pale mtu unapofanya kitu ili tu uwe na kitu cha kufanya na siyo kufanya kitu kwa sababu ni sahihi na muhimu kufanya.
Makosa mengi ambayo watu wamekuwa wanayafanya, chanzo chake ni mtu kutaka tu kufanya kitu, ili ajiridhishe kuna kitu anafanya na pia aonekane na wengine kuna kitu anafanya.
Rafiki, maisha siyo mashindano au maonesho ya nani anafanya nini, maisha ni kujua nini unataka na jinsi gani utapata unachotaka na kisha kuweka juhudi kukipata. Kama imefika mahali huna cha kufanya, kaa na tulia mpaka pale utakapokuwa na cha kufanya. Usilazimishe kufanya chochote ili tu uwe na cha kufanya, kwa sababu utatengeneza matatizo ambayo yatakutaka ufanye zaidi na zaidi, unapokuna kustuka unakuta umeshaacha kile ulichokuwa unataka na unahangaika kutatua matatizo uliyozalisha kwa kufanya vitu hivyo.
Kuwa mvumilivu pale unapokuwa unasubiria fursa fulani inayochelewa, zuia tamaa ya kufanya chochote ili tu uonekane una kitu unafanya. Usikimbilie kufanya maamuzi ya haraka kwenye jambo lolote. Hii ndiyo njia pekee ya kupiga hatua kwenye maisha na kupunguza matatizo na changamoto.
Watu wengi wamekuwa wanachanganya kuwa ‘bize’ na kuzalisha, unaweza ukawa bize kweli, lakini hakuna unachozalisha. Na unaweza kuwa na uzalishaji bora bila ya kuwa bize. Muhimu ni kujua unachotaka na njia bora ya kukipata kisha kufanya hayo pekee na kuachana na mengine.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,