Tuna nyakati tatu,
Wakati uliopita, huu umeshapita, hatuwezi kuubadili kwa namna yoyote ile. Ila tunaweza kujifunza kwenye wakati uliopita na kuwa bora zaidi leo na kesho.
Wakati uliopo, huu ni wakati ulionao sasa, wakati pekee unaoweza kuutumia kufanya chochote unachotaka kufanya.
Wakati ujao, huu ni wakati ambao bado hatujaufikia, hivyo hatuwezi kuuathiri kwa namna yoyote ile.
Sasa matatizo mengi ambayo watu wamekuwa wanayapata yanatokana na kushindwa kutumia vizuri nyakati hizi tatu. Wengi wanapoteza wakati walionao, kwa kufikiria na kujutia wakati uliopita na kuhofia wakati ujao.
Kitu sahihi kwako kufanya ni kutawala wakati uliopo, kujifunza kwenye wakati uliopita na kuwa na maandalizi bora kwa wakati ujao.
Wakati uliopita jifunze kwa uzoefu wako na wa wengine. Angalia mazuri uliyofanya na yarudie, makosa uliyofanya na yaepuke. Kadhalika kwa wengine, angalia mazuri yaona yaige, makosa yao yaepuke. Ni muhimu sana kujifunza kupitia wengine kwa sababu huwezi kujua kila kitu mwenyewe na ukisema usubiri mpaka ujifunze kwa uzoefu wako mwenyewe, utachelewa sana.
Kwa wakati ujao, kuwa na maono makubwa, kuwa na picha kubwa ambayo unataka kuifikia, kuwa na matumaini kwenye kuifikia picha hiyo na usikubali kuyumbishwa na chochote.
Na kwa wakati ujao, ni KAZI TU, chukua hatua sasa. Kitakachokufikisha unakotaka kwa kutumia uzoefu ulionao, ni hatua unazochukua sasa, na siyo unachojua au kutamani.
Kila siku fanya kitu, piga hatua ya kukusogeza karibu zaidi na mafanikio makubwa unayoyatazamia.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,