“Leisure without study is death—a tomb for the living person.”
—SENECA, MORAL LETTERS, 82.4
Tunapaswa kushukuru sana kwa nafasi hii nyingine nzuri tuliyoiona leo,
Siyo wote waliopanga kuiona siku hii wameweza kuiona, tuna bahati ya kipekee na tunapaswa kuitumia kwa kufanya yale yaliyo sahihi kwetu na kwa wengine.
Msingi wetu ni NIDHAMU, UADILIFU NA KUJITUMA,
Mwongozo wetu ni AFYA, UTAJIRI NA HEKIMA,
Msimamo wetu ni KAZI, UPENDO NA HUDUMA.
Kwa kusimamia maeneo hayo matatu, siku ya leo itakuwa bora sana kwetu.
Asubuhi ya leo tutafakari MAPUMZIKO BILA KUJIFUNZA NI KIFO….
Unaweza kuchagua kuwa na siku ya mapumziko kwenye kazi yako,
Lakini kamwe hupaswi kuchagua kuwa na siku ya mapumziko kwenye kujifunza.
Kwamba unachagua siku ambayo itakuwa ni ya starehe tu kwako, hufanyi chochote ambacho ni kazi na wala hujifunzi chochote.
Siku hiyo kwako ni kulewa, kubarizi ufukweni, kucheza muziki, kuangalia tamthilia na mengine.
Unaweza kuona hayo ndiyo mapunziko sahihi, yanayokufanya uisahau kazi kwa muda, lakini ni kifo unakitengeneza, kaburi ndani ya mwili wako ulio hai.
Kwenye maisha kuna kwenda mbele au kurudi nyuma, hakuna kusimama. Kuna kukua au kufa, hakuna kubaki pale pale.
Hivyo kama mtu hajifunzi, maana yake hakui na kama hakui basi anakufa.
Ndiyo maana unapochagua kutokujifunza, unakuwa umechagua kufa. Unaweza kuonekana upo hai kimwili na unachangamana na wengine, lakini kiroho na kiakili ni mfu, upo tu kama msukule.
Wasiojifunza kila siku hawana tofauti na misukule, angalia hata wanavyofanya mambo yao na kuishi maisha yao. Hawafikiri chochote, wanaangalia jana wamefanya nini na wanafanya hicho hicho leo. Wanaangalia wengine wanafanya nini na wao wanafanya pia. Hawana maamuzi yao binafsi kwa sababu hawajui jinsi ya kufikia maamuzi hayo, kwa kuwa hawajifunzi.
Chagua kuwa mwanafunzi maisha yako yote, kwamba kila siku unayokuwa hai, ni siku ya wewe kujifunza.
Kila unapokwenda, unakuwa na kitabu karibu yako, na unatenga muda wa kukisoma pia.
Kila unapopata nafasi ya kutembelea eneo lolote lile, hakikisha unajifunza vitu ambavyo hukuwa unavijua kuhush eneo hilo.
Kila unapokutana na mtu yeyote yule, swali kuu unalopaswa kujiuliza ni kitu gani naweza kujifunza kutoka kwa mtu huyu. Na kila mtu ana kitu ambacho unaweza kujifunza kutoka kwake.
Kuwa mdadisi, kuwa msikilizaji na kuwa mtazamaji, utajifunza mengi popote unapokuwa na kwa chochote unachofanya.
Ukawe na siku bora sana ya leo, siku ya kujifunza ili kuendelea kuwa hai kimwili, kiakili na kiroho.
#KilaSikuJifunze #UnapofikiriUnajuaKilaKituNdiyoHujuiChochote #KuwaMwanafunziWaMaisha
Wako rafiki katika safari ya kuelekea mafanikio makubwa,
Kocha Dr Makirita Amani,
http://www.amkamtanzania.com/makirita3.1