Kinachotuponza tusiyafurahie maisha yetu ni kujidanganya sisi wenyewe.
Tumekuwa tunajidanganya kwenye mambo mengi, ambayo kama tusingefanya hivyo, tungepata nafasi ya kuyaishi maisha yetu vizuri na kuyafurahia.
Moja ya maeneo ambayo tumekuwa tunajidanganya ni kwenye urefu wa maisha, huwa tunajiambia tunataka kuishi maisha marefu. Tunahangaika na mambo mengi ya kurefusha maisha.
Lakini hatujawahi kukutana na mtu mwenye miaka elfu moja, au mia tano, au mia mbili. Wengi ambao tunasikia wameishi miaka mingi, ni mia moja na kidogo.
Sasa rudi kuangalia umri wa dunia, haijalishi unatumia mahesabu gani, utaishia kwenye ukweli kwamba dunia ina miaka mingi mno ukilinganisha na umri ambao binadamu mmoja mmoja anaweza kuishi.
Ukihesabu kwa kutumia vitabu vya kidini, utapata kwamba dunia ina miaka zaidi ya elfu 4, sasa linganisha na miaka 100 ambayo mtu anayeishi muda mrefu anakuwa ameishi, ni kidogo sana.
Ukihesabu kisayansi, dunia ina miaka zaidi ya bilioni 9, ukilinganisha na maisha marefu ambayo mtu anaweza kuishi, ni kichekesho.
Lengo la makala hii ya leo siyo kudharau mpango wowote ulionao wa kuishi miaka mingi, bali kujiweka kwenye fikra na mtazamo sahihi na kuacha kujidanganya. Lakini pia kutumia vizuri muda ulionao sasa, kuishi maisha kamilifu kwako badala ya kuahirisha maisha ukiamini utapata muda zaidi kesho au siku zijazo.
Hakuna anayejua ni miaka mingapi anayo ya kuishi hapa duniani.
Lakini pia, hata atakayeishi miaka mingi zaidi, bado ni michache sana ukilinganisha na umri ambao dunia imeishi.
Na kwa hakika, miaka 100 ijayo, kila anayesoma hapa leo, atakuwa amekufa, haijalishi ni nani au anafanya nini, wote tutakuwa tumekufa.
Hivyo tuwe wanyenyekevu na tutumia muda tulionao kuyaishi maisha yetu kwa ukamilifu, hatujui kama tutapata muda mwingine kama huu.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,