SheriaYaLeo (43/366); Rudia rudia kufanya.

Mfumo wa elimu unafundisha vitu kwa nadharia, kwa mwanafunzi kusoma na kufanya mitihani.
Katika kipindi chote cha elimu mwanafunzi anajifunza kwa kupewa maarifa na taarifa tu.

Haishangazi kwa nini mwanafunzi anapohitimu masomo na kwenda kwenye dunia halisi anajikuta hakuna anachoweza kufanya.
Anaweza kuwa na vyeti vyenye ufaulu mkubwa, lakini hakuna anachoweza kufanya.

Unajifunza vyema kupitia kufanya kwa vitendo yale unayojifunza.
Na tena siyo tu kwa kufanya mara moja, bali kwa kurudia rudia kufanya kwa muda mrefu.
Ubobezi unajengwa kupitia kurudia rudia kufanya kitu.

Kwa kuweka umakini mkubwa kwenye kile ambacho mtu unajifunza na kwa kurudia rudia kufanya kwa muda mrefu, huku ukijaribu vitu vipya kila wakati, utaweza kujijengea ubobezi mkubwa.

Kwa kurudia rudia kufanya kwa muda mrefu unafika hatua ambayo ubongo wako unaweza kufanya bila hata ya kufikiria sana.
Pale unapowaona watu wakifanya kitu na ukashangaa, siyo kwamba wamezaliwa wakiwa wanajua kufanya kitu hicho, ila wamejifunza na kufikia ubobezi kwa kurudia rudia kufanya kwa muda mrefu.

Sheria ya leo; Ubongo wetu umetengenezwa kujifunza kitu kwa kwa kurudia rudia kufanya kwa muda mrefu. Kupitia ufanyaji huo wa kurudia rudia, ujuzi wowote unaweza kujengwa. Chagua ni ujuzi gani unaotaka kujijengea na anza kujifunza kwa kurudia rudia kufanya.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu