2839; Kukosa cha kufanya.
Watu huwa wanapoteza muda kwa sababu wanakuwa hawana kitu kingine cha kufanya.
Wengine wanatengeneza hata matatizo kwa sababu tu hawana cha kufanya.
Kikubwa ambacho naendelea kujifunza kwenye maisha yetu wanadamu ni kwamba muda hauwezi kukaa mtupu, lazima kuna kitu kitajipenyeza tu.
Hivyo basi, kama kweli unataka kufanya makubwa kwenye maisha yako, pangilia muda wako wote kwa vitu ambavyo ni muhimu kuvifanya.
Na ili uvifanye kweli, hakikisha kuna maumivu unayapata kama hutafanya.
Wote tuna mifano hai kwetu wenyewe. Umewahi kuwa na jukumu ambalo lilikuwa na muda mrefu wa kulifanya na hukuwa unalifanya sana, uliahirisha huku muda ukipotelea kwenye vitu vingine.
Lakini pale jukumu hilo lilipofikia mwisho wa kufanyika, ulipata muda wa kulifanya na kulikamilisha kwa wakati.
Hicho ni kiashiria kizuri kwamba unaweza kufanya mambo makubwa na kwa wakati.
Hivyo basi, pangilia mambo yako kwa namna ambayo utalazimika kuyafanya kwa muda uliotenga.
Kwa sababu usipofanya unaumia.
Unaweza kuwaahidi watu kitu kitakuwa tayari mapema na kama hutakamilisha basi wakutoze faini fulani au badala ya kukulipa watakipata bure. Hilo linakusukuma hasa.
Au unaweza kuwa na kocha anayekusimamia kwa karibu na kuhakikisha kweli unafanya, hakuachii kirahisi usifanye. Kocha anatumia kila njia kuhakikisha kweli unafanya bila kuacha.
Hatua ya kuchukua;
Vitu gani muhimu umekuwa unapanga kufanya lakini unajikuta unakosa muda wa kuvifanya? Panga sasa namna utavifanya na tafuta mtu wa kukusimamia ufanye kama ulivyopanga. Na ukienda nje ya mpango wako atekeleze adhabu uliyoahidi.
Tafakari;
Watu wapo ‘bize’ muda wote lakini bado hawakamilishi yale muhimu. Ni kwa sababu wanakosa nidhamu kali kwenye kupanga yaliyo muhimu kufanya na kusimamia mipango waliyoweka. Kinachotokea ni mengi yasiyo muhimu yanajipenyeza kwao na kujikuta wakichoka sana huku hakuna hatua wanazopiga.
#LetsBuildBusinesses
#NothingElseMatters
#BillionairesInTraining
#WeAllGonnaMakeIt
#WorkHardAndYouWillSucceed