3007; Jaribio.

Rafiki yangu mpendwa,
Moja ya vikwazo vikubwa kwa watu kufanikiwa ni tabia ya kughairisha mambo.
Mtu anakuwa anajua kabisa nini anatakiwa kufanya, lakini hafanyi.

Na mara nyingi sana kinachowafanya watu waghairishe mambo ni kuyaona ni makubwa na kuhofia kushindwa.
Mambo yanayoghairishwa zaidi ni yale ambayo ni mapya na makubwa.

Yanaghairishwa kwa sababu mtu anaona ni magumu na uwezekano wa kushindwa ni mkubwa.
Hivyo anaona ni bora kufanya yaliyozoeleka hata kama matokeo yake ni madogo.

Rafiki, sayansi imeweza kukua sana kwa sababu moja; majaribio.
Sayansi imekuwa inatoa nafasi kwa kila mtu kufanya majaribio bila kuhofia ukubwa au kushindwa.

Yeyote anayekuwa na wazo la kitu kipya, sayansi inampa uwanja wa kufanyia majaribio mawazo hayo na kuona ni matokeo gani yanapatikana.

Na wakati wa jaribio, mtu anafanya kila kitu kwa uhakika na kukusanya taarifa zote zinazopatikana.
Ni taarifa na matokeo ndiyo yanaamua kama wazo aliloanza nalo mtu ni sahihi au la.
Kama ni sahihi linaendelea kutumika na kama siyo sahihi linaendelea kufanyiwa maboresho kwa majaribio mengine zaidi.

Kinachowakwamisha wengi kwenye hii safari ya mafanikio ni kuogopa ukubwa na upya wa vitu ambavyo watu wanajifunza na kutakiwa kufanya.
Watu wanakuwa na mawazo mazuri sana, ambayo ni mapya na makubwa sana.
Lakini inapofika kwenye kuyatekeleza mawazo hayo wanasita, kwa kuhofia kushindwa.

Njia bora ya kuvuka hofu hiyo na kufanya mambo hayo mapya na makubwa ni kuchukulia kila kitu kama jaribio.
Chukulia unajaribu wazo hilo jipya kwa kipindi cha muda fulani.
Katika kipindi hicho cha majaribio, unafanya kila kinachopaswa kufanyika bila ya kuhofia kushindwa.
Unachukulia kama ni kitu cha uhakika na unafanya bila ya kujizuia kwa namna yoyote ile.
Na hapo unakusanya taarifa nyingi ya nini kinafanya kazi na nini hakifanyi kazi.

Unakwenda hivyo ukiboresha matokeo yanayopatikana bila kuhofia au kukwamishwa na chochote kinachoendelea.

Kwa kuchukulia mambo kwa mtazamo huu wa majaribio, inaondoa ule msongo unaokuwepo kwenye mambo mapya na kukupa uhuru mkubwa wa kuyafanya.
Inafanya kushindwa kusiwe kitu kikubwa na kinachoumiza, kwa sababu ni jaribio unafanya.
Inakupa ujasiri wa kujaribu mambo ambayo katika hali ya kawaida usingethubutu kufanya hivyo.

Kwa jambo lolote kubwa na jipya unalotaka kufanya lakini hofu inakuzuia, lifanye kama jaribio.
Jipe kipindi cha angalau miaka 2 ambapo utafanya jambo hilo kama kujaribu na uone matokeo gani utayapata.
Katika kipindi hicho kama matokeo yatakuwa mazuri unaendelea. Na kama matokeo yanakuwa siyo mazuri unaboresha wazo la mwanzo au matokeo yanayopatikana.

Muhimu ni wakati unafanya kitu kama jaribio, usifanye nusu nusu, badala yake ingia mazima, fanya kwa uhakika hasa. Fanya kwa namna kinavyopaswa kufanyika bila ya kujikwamisha kwa namna yoyote ile.
Jitoe kweli kama ni kitu una uhakika nacho na angalia matokeo yanayopatikana.
Nenda ukiboresha matokeo hayo na kufanya kwa juhudi zaidi bila kuchoka wala kuleta mazoea.

Kwa kwenda hivi, utaweza kufanya makubwa sana kwenye maisha yako na kupata chochote unachotaka.
Maisha yenyewe ni majaribio, hakuna chochote cha uhakika, hata yale ambayo ni mazoea.
Uhakika wowote tunaojipa ni kujidanganya tu.

Wewe yafanye maisha yako kuwa ya majaribio na utakuwa na fursa za kupiga hatua zaidi.
Lakini yasiwe majaribio ya kila wakati kuanza vitu vipya na kuishia njiani, hasa pale unapokutana na kitu kingine kipya.
Bali yanapaswa kuwa majaribio ya kuchukua kitu kipya, kukifanyia kazi kwa uhakika kwa kipindi fulani bila ya kuacha au kukimbilia kwenye mambo mengine.

Kuchukulia kitu kama jaribio kunaondoa ile hofu ya kushindwa kwenye vitu vipya na vikubwa na hivyo kukupa uhuru wa kufanya. Hata kama utashindwa, utajua ulikuwa unajaribu, hivyo hutakata tamaa, badala yake utaboresha zaidi. Na hivyo ndivyo unavyoweza kujenga mafanikio makubwa kwenye maisha yako.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#BilioneaMafunzoni
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe