3204; Usimwache akapoa.

Rafiki yangu mpendwa,
Mara baada ya mteja kununua kwako, nini huwa kinafuata?
Kwa walio wengi, mteja anaponunua muuzaji anafurahia hayo mauzo kisha kumshukuru na kumwacha aende zake.

Hili ni kosa kubwa ambalo limekuwa linawanyima wauzaji fursa ya kufanya mauzo mengi zaidi.
Mara baada ya mteja kununua, huwa anakuwa kwenye moto wa kuendelea kununua zaidi.
Lakini hilo litategemea uwezo wa muuzaji kumshawishi mteja kufanya manunuzi ya ziada mara baada ya kukamilisha mauzo makuu.

Kuna sababu mbili ambazo zinawafanya wateja kuwa tayari kufanya manunuzi ya ziada.
Moja ni kuwa na fedha, hii iko wazi, watu wengi wanapokuwa na fedha huwa hawapati utulivu mpaka fedha hizo zimeisha. Hivyo watu wanapokuwa wamefanya manunuzi na bado wana fedha, wanakuwa na msukumo wa kuendelea kufanya manunuzi zaidi.

Mbili ni kujisikia vizuri, ambapo watu wanapokuwa wanajisikia vizuri baada ya manunuzi, wanakuwa na msukumo wa kuendelea kufanya manunuzi zaidi.
Tunajua jinsi ambavyo manunuzi ya maandishi huwa siyo ya mantiki bali ya hisia. Pale mtu anapojisikia vizuri anapata msukumo wa kununua zaidi.

Hivyo basi, ili uweze kunufaika na nguvu hiyo ya wateja kufanya manunuzi zaidi, kuna vitu viwili unavyopaswa kuvifanya kwa uhakika kwa kila mteja wako.

Kitu cha kwanza ni kuwahudumia wateja vizuri sana pale wanapokubali kununua. Lengo hapa ni kuwafanya wateja wajisikie vizuri ili waendelee kununua.
Ipo ndani ya uwezo wako kuwafanya wateja wajisikie vizuri, ndiyo wajibu wako namba moja kama muuzaji.

Kitu cha pili ni kuchagua kitu cha ziada ambacho utamshawishi mteja aweze kukinunua pia ili manunuzi yake ya kwanza yawe na tija.
Mfanye aone manunuzi ya kwanza hayajakamilika kama hajafanya manunuzi ya ziada.
Hili linakuwa rahisi kufanya kama unaijua biashara yako vizuri.

Kitu muhimu sana kinachopaswa kufanya ni kuibua tamaa ndani ya mteja ili aendelee kufanya manunuzi.
Bila ya kuibua tamaa, msukumo wa mteja kufanya manunuzi ya ziada unakuwa mdogo.

Kama utaibua tamaa ndani ya mteja lakini usimfanyie mauzo ya ziada, ataenda pengine na kufanya hayo manunuzi.
Hivyo kama utamwonea mteja huruma kwa kuona inabidi umwachie fedha alizonazo, hatabaki nazo kwa muda mrefu. Kuna muuzaji mwingine atazichota kurahisi sana, tena bila hata ya kufanya kazi kubwa.

Kama muuzaji unapaswa kuwa na mkakati wa kuwashawishi wateja kufanya manunuzi ya ziada kila unapowauzia.
Mkakati wako unapaswa kuwa na hatua kadhaa, mfano;

1. Baada ya mteja kukubali kununua bidhaa/huduma kuu aliyofuata, unampendekezea bidhaa/huduma nyingine inayoenda pamoja na kuu aliyonunua.
Hii ni hatua unayopaswa kufanya kwa kila mteja anayenunua, usimwache hata mmoja.

2. Anzisha naye mawasiliano ya haraka baada ya manunuzi, iwe amekubali kufanya manunuzi ya ziada au la.
Unaanza kwa kumtumia salamu za shukrani kwa yeye kununua kwako, salamu hizi zinatumwa ndani ya masaa 24 tangu kununua kwake.
Kisha ufuatiliaji wa karibu wa mteja unaendelea, kwa mteja kuendelea kupewa taarifa za vitu vilivyopo na vinaendana na manunuzi ambayo tayari ameshayafanya.

Kama muuzaji, wajibu wako namba moja ni kuuza.
Hivyo kwa kila mteja ambaye ameshanunua karibuni, anapaswa kuwa kwenye mchakato wako wa kumfanyia mauzo zaidi na zaidi.
Mahitaji mengi ya wateja huwa hayaishi, kadiri tamaa inavyoibuka ndani yao, ndivyo wanavyosukumwa kununua zaidi.
Kama hutawauzia wewe, kuna wengine watawauzia.

Ili uweze kufanya mauzo makubwa zaidi kwa kila mteja, usimwache akapoa. Wakati ana moto wa manunuzi, endelea kuuchochea huo moto ili afanye manunuzi zaidi.
Amebaki na kiasi gani cha fedha huo siyo wajibu wako.
Wajibu wako ni kuendelea kumfanya mteja ajisikie vizuri na kuibua tamaa ya kuendelea kununua.

Kama unataka kuwa na mashine itakayokuingizia fedha bila ya ukomo, basi ni mauzo.
Na ili mauzo ya kuingizie fedha bila ukomo, yafanye kwa mkakati sahihi.
Mara zote wafanye wateja wajisikie vizuri kisha ibua ndani yao tamaa ya kufanya manunuzi zaidi.
Kamwe hupaswi kumwacha mteja akapoa, badala yake endelea kumchochea moto ili umfanyie mauzo makubwa zaidi na zaidi.

Kwa vyovyote vile, usiache kuuza.
Huo ndiyo wajibu wako mkuu hivyo ufanye kwa uhakika.
Na kamwe usipate fikra za kumwachia mteja kiasi fulani cha fedha.
Wewe siyo mshauri wala msimamizi wa fedha za wateja wako.
Wewe unawajibika kuwapa wateja bidhaa/huduma ambazo zina thamani kubwa kwao na zinayafanya maisha yao kuwa bora.
Halafu wao watajua wenyewe jinsi ya kupangilia na kusimamia fedha zao binafsi.

Uza.
Uza tena.
Na uza tena na tena na tena.
Kamwe usiache kuuza kwa mteja ambaye ameshanunua kwako.
Hayo ni mauzo rahisi zaidi unayoweza kuyafanya, kama mambo mengine yote umeyafanya kwa usahihi.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe