3219; Ubora na Mafanikio makubwa.

Rafiki yangu mpendwa,
Watu wengi wanayapenda mafanikio makubwa.
Lakini wengi hawayapati, siyo kwa sababu hawawezi kuyapata, bali kwa sababu hawajui namna sahihi ya kuyapata.

Tunajua umuhimu wa kuweka kazi kwa msimamo na muda mrefu ili kufanikiwa.
Na wapo wengi wanaoweka sana kazi na kwa muda mrefu bila kuacha, lakini bado hawayapati mafanikio makubwa wanayoyataka.

Kazi, muda, msimamo na ung’ang’anizi ni vitu vyenye mchango muhimu kwenye mafanikio makubwa ambayo mtu anataka kuyapata.
Lakini peke yake haviwezi kumpa mtu mafanikio makubwa kabisa.
Vinaweza kuchangia mafanikio ya wastani, lakini yale ambayo ni makubwa zaidi, kuna kitu kingine kinachohitajika kutangulia.

Kitu hicho ni kuwa bora sana kwenye kile unachofanya kiasi kwamba watu hawana pengine pa kwenda ila kwako.
Pale watu wanapokuwa wanataka kitu hicho kwa uhakika wanakuwa hawana pengine pa kwenda ila kwako tu.

Watu wengi huwa hawazingatii sana msingi huu muhimu, kwa sababu kuwa bora sana kunataka juhudi kubwa na muda, wakati kuwa kawaida bado kunawalipa.
Hivyo wanalewa mafanikio madogo wanayoyapata kwa kuwa kawaida, lakini hawajui wamejizuia kupata mafanikio makubwa zaidi kama wangekuwa bora.

Iko hivi, unapokuwa unafanya kitu kwa ukawaida, unapata watu wa kawaida pia ambao wanakihitaji.
Hivyo siyo kwamba utakosa kabisa mafanikio.
Tatizo linakuja kwamba unapokuwa kawaida, huwezi kutoza gharama kubwa, kwa sababu watu wanaweza kupata kwa wengine hicho hicho wanachopata kwako na kwa gharama ndogo.

Kwa sababu ushindani ni mkali na kila mara kuna watu wapya wanaingia, ambao wapo tayari kutoza gharama ndogo, njia pekee ya kupata mafanikio makubwa ni kuwa bora sana kiasi cha kutegemewa.

Watu wengi wanashindwa kupata mafanikio wanayoyataka kwa sababu hawawezi kutoza gharama kubwa.
Na wanashindwa kutoza gharama kubwa kwa sababu hawana ubora mkubwa kwenye kile wanachofanya.
Kwa bahati mbaya sana, hilo linazidi kuwadidimiza.

Ukiwa bora kabisa, hakuna anayetegemea pia uwe rahisi zaidi. Watu wanapoenda kwa aliye bora kuliko wote, wanajua kabisa watalazimika kulipa zaidi.
Kadhalika kama gharama unayotoza ni ndogo zaidi, hakuna anayetegemea utakuwa bora zaidi. Watu wanajua kwa gharama ndogo unayotoza, huwezi kuwapatia kile kilicho bora.

Hivyo unajionea mwenyewe kwa nini kuwa bora kabisa ni kitu ambacho hakikwepeki kama unataka kujenga mafanikio makubwa na yanayodumu.

Wajibu wako mkubwa ni kila wakati kuwa unajiuliza unawezaje kuwa bora zaidi ya ulivyo wakati huo.
Kwa sababu swala siyo tu kuwa bora, bali kuendelea kuwa bora zaidi kila wakati.
Kwa sababu kama ambavyo tumeshaona, watu wapya wanakuja kila wakati.
Sasa kama wewe hutakuwa na tofauti na watu hao wapya, hutaweza kupata mafanikio makubwa unayoyataka.

Ili kuwa bora na kuendelea kuwa bora, unahitaji pia kupenda sana kile unachokifanya na kukitoa kukifanya kwa viwango vya juu kabisa bila ya kuacha.
Unapoweka kila ulichonacho kwenye kile unachofanya, hakuna namna utashindwa kupata mafanikio makubwa.
Yaani unakuwa umejiweka kwenye nafasi kwamba kitu pekee kitakachotokea kwako ni mafanikio makubwa pekee.

Yaani unakuwa huna hata wasiwasi, kwa namna unavyokuwa umejitoa, kwa mapenzi na juhudi kubwa unazokuwa umeweka na namna unavyoendelea kuwa bora, mafanikio yanakuwa ni swala la muda tu.
Hujiulizi kama utafanikiwa au la, unachokuwa unasubiri ni wakati wako wa kuyavuna mafanikio.

Jambo muhimu sana la kujiambia mara zote ni hili; “Hapa ndipo nilipo. Nakwenda kuwa hapa. Nitakuwa bora zaidi.”
Ukijiambia na kuiishi kauli hii mara zote, hakuna namna utakosa mafanikio makubwa.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe