3239; Utawatambua kwa matendo.

Rafiki yangu mpendwa,
Ni rahisi sana kujua kama mtu atapata mafanikio makubwa kwenye maisha yake au la.
Na njia ya kufanya hivyo siyo kusikiliza watu wanasema nini, bali kuangalia wanafanya nini.

Kama anachosema mtu ni tofauti na anachofanya, amini kile anachofanya, maana huo ndiyo ukweli.

Wanaofanikiwa na wanaoshindwa utaweza kuwatambua kwa matendo yao.
Matendo ndiyo yenye nguvu kubwa kwenye kuamua maisha ya mtu yanakuwaje.

Kwa watu ambao mara zote wana usumbufu mwingi, wanafanya vitu vingi kwa wakati mmoja, ni dhahiri kwamba hawawezi kupata mafanikio makubwa.
Kwa sababu nguvu wanazozitawanya kwenye mambo mengi kama wangezikusanya kwenye eneo moja wangezalisha matokeo makubwa zaidi.

Huhitaji uwe na akili nyingi sana kutambua kwamba mtu anayekimbizana na fursa mpya kila wakati ni mtu ambaye pia hawezi kufanya makubwa.
Kwa kila wakati mtu kuwa anaanza kitu kipya anakuwa anapoteza nguvu kubwa ambayo hawezi kuitumia kwenye kupata matokeo mazuri.

Tumekuwa tunaambiana hili mara kwa mara na hapa nalirudia tena ili liweze kunasa kweli kweli.
Kwa chochote unachotaka kupata kwenye maisha yako, anza kwa kuangalia wale ambao tayari walishakipata hicho.
Kisha angalia jinsi walivyofanya mpaka kupata walichotaka.
Utajifunza mengi sana kupitia waliyofanya.

Kosa kubwa ambalo wengi wamekuwa wanafanya na linawagharimu ni kuangalia kile ambacho watu wanafanya baada ya kuwa wameshapata kile walichokuwa wanataka sana.
Kilichokuwa kinawasukuma watu wakati wanaanzia chini kabisa huwa ni tofauti na kinachoendelea kuwasukuma baada ya kuwa wamepata kile walichotaka.

Jifunze kwa wengine kwa kuangalia matendo.
Na jihakikishie ushindi na wewe kwa kuwa mtu wa vitendo sahihi.
Vitendo ni vya ukweli kuliko maneno mengine yoyote ambayo mtu anaweza kuyatoa.
Tumia matendo kufanya maamuzi sahihi.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe