3349; Gereza la kujitakia.

Kutoka mezani kwa Kocha,

Rafiki yangu mpendwa,
Katika viumbe wote waliopo hapa duniani, binadamu ndiye kiumbe mwenye uwezo mkubwa sana wa kuwa na kufanya vile anavyotaka yeye.

Viumbe wengine wanazaliwa wakiwa tayari wameshaandaliwa jinsi gani watakuwa na watafanya.
Na wanakuwa hawana uhuru wa kubadili vile walivyopangiwa.

Fikiria kama mti ambao umeota eneo fulani na unatoa matunda ya aina fulani. Hauwezi kujiamulia tu wenyewe kuhama au kutoa matunda ya aina tofauti.
Lakini binadamu tuna uhuru wa kuhama popote tulipo na kutoa vitu vya tofauti.

Kadhalika ukimwangalia mnyama kama swala, atayaishi maisha yake aliyopangiwa kama swala, hakuna anachoweza kubadili.
Ila sisi binadamu tunayo mengi sana tunayoweza kubadili.

Cha kushangaza sasa, pamoja na uwezo huo mkubwa tulionao, pamoja na uhuru wa kuwa vile tunavyotaka, sisi wenyewe tumechagua kujiweka kwenye magereza ya kujitakia, funguo za magereza hayo tukiwa nazo sisi wenyewe.

Magereza ambayo tumejiweka ni ukomo tunaojiona tunao kwenye maeneo mbalimbali ya maisha yetu.
Licha ya uwezo mkubwa tulionao, hatuutumii na matokeo yake ni kushindwa kufanya makubwa.
Tunaweza kulaumu wengine kwa namna mbalimbali, lakini chanzo kikuu ni sisi wenyewe kushindwa kutumia uwezo mkubwa wa ndani yetu.

Kama twiga angepewa akili zetu binadamu, angeishia kimo cha swala. Angejiweka kwenye gereza la kwamba  hawezi kwenda zaidi ya hapo.
Angejiambia akiwa mrefu sana atakosa majani mazuri.
Na mengine ya aina hiyo.
Hivyo ndivyo binadamu tunavyojiweka kwenye magereza ya kujitakia, na kushindwa kufanya makubwa.

Wanyama ambao hawana uwezo kama wetu wanaweza kufanya makubwa kwa sababu akili zao haziwezi kutengeneza magereza tunayojitengenezea sisi.

Kwenye jamii ya KISIMA CHA MAARIFA, ambayo ni jamii ya tofauti tunayoijenga, tunavunja kila aina ya gereza ambalo tumejiweka.
Kila tunachojiambia hatuwezi kufanya, ndiyo hicho tunakifanya zaidi.
Kila tunapojiambia tumechoka, ndiyo tunaongeza juhudi zaidi.
Kila tunapojilinganisha na wengine, tunajikumbusha tunaweza kufanya makubwa zaidi.
Kwa kujisukuma zaidi ya pale tulipo kwa kila wakati, tunatumia uwezo wetu mkubwa na kuondoka kwenye kila aina ya gereza tunalokuwa tumejiweka.

Vunja kila aina ya gereza ili uwe huru na kufanya makubwa kwenye maisha yako.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe