Katika kurasa zilizopita, tuliona ya kwamba hakuna mtu anaweza kuibukia kileleni. Badala yake unahitaji kupanda hatua moja baada ya nyingine ndipo ufike kileleni. Na pia tuliona safari hiyo siyo rahisi, ndiyo maana wengi huwa wanaishia njiani. Unaweza kuisoma hapa; UKURASA WA 451; Kuibukia Kileleni…

Sasa kuna kitu kimoja ambacho hatukukiangalia kwenye kupanda mlima na kufika kileleni. Kwa sababu bila ya kukijua kitu hiki unaweza kujikuta unakata tamaa. Ni rahisi kuona kama nikikazana na kumaliza kupata mlima huu basi mambo yangu yatakuwa vizuri sana. Lakini huo sio ukweli, kwa sababu….

Baada ya kumaliza kupanda mlima mmoja, unakuta kuna milima mingine mingi inakusubiri upande. Siyo kwamba ukishapanda mlima mmoja basi mambo yako yamekwisha, bali unahitaji kupanda milima mingine mingi zaidi.

Hivi ndivyo maisha yalivyo, ukimaliza kufanyia kazi jambo moja, unaona kuna mengine tena ya kufanyia kazi. Ukimaliza kutatua changamoto moja, unaona kuna changamoto nyingine nyingi zinakusubiri uzitatue.

Hakuna siku utasema nimemaliza milima yote na sasa nakaa kileleni tu, kila siku kutakuwa na milima mingine ya kupanda.

Na la kuelewa zaidi ni kwamba kila mlima utakutana na changamoto zake katika kuupanda.

Haya ndiyo maisha, tangu kuzaliwa mpaka kufa kwako, ni safari ya kupanda milima. Ni vyema ukafurahia safari hizi na sio kusubiri mpaka ufike kileleni, maana kila baada ya kilele kuna mlima mwingine.

SOMA; Sheria 65 Za Mafanikio, Furaha Na Maisha Bora Kutoka Kwa ROMAN.

TAMKO LANGU;

Nimejua ya kwamba nikishamaliza kupanda mlima mmoja, kuna milima mingine mingi inanisubiri kupanda. Nimejua maisha ni kupanda milima, tangu kuzaliwa mpaka kufa. Nimejitoa kupanda milima hii na nitafurahia kila safari badala ya kusubiri nifike kileleni.

NENO LA LEO.

After climbing a great hill, one only finds that there are many more hills to climb. – Nelson Mandela

Baada ya kupanda mlima mmoja, ndipo unapogundua ya kwamba kuna milima mingi zaidi ya kupanda.

Kuna milima mingi ya kupanda kwenye maisha yako, jifunze kufurahia safari na siyo kusubiri mpaka mwisho wa safari, maana hakuna mwisho mpaka utakapokufa.

Rafiki na Kocha Wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz

TUPO PAMOJA.