Kama unataka kuwa na maisha ya kushindwa, kuwa na maisha ya kawaida, maisha ambayo unafanya kile ambacho kila mtu anafanya, kwa namna anavyofanya. Yaani unakuwa kawaida kabisa, na hakuna hatua kubwa unayopiga.

Ukifanya biashara yako kama kawaida, vile ambavyo umezoea kufanya siku zote, na vile ambavyo kila mtu anafanya, unakuwa umechagua wewe mwenyewe kushindwa. Unakuwa umechagua kubaki nyuma kwenye dunia inayoenda mbele kwa kasi kubwa.

Kama unafanya kazi yako kwa ukawaida, vile ambavyo kila mtu amekuzoea kufanya na vile ambavyo kila mtu anategemea kupata kutoka kwako, jua unatengeneza mazingira ya kushindwa.

Haijalishi unakazana kiasi gani, unapokubali kuwa kawaida, unapofanya kile tu ulichozoea, kushindwa ni lazima.

Mambo ya Kawaida

Watu wa kawaida, wanaofanya mambo yao kawaida huwa hawana chochote kikubwa cha kuonesha, kwa sababu kawaida inazalisha matokeo ambayo ni ya chini kabisa.

Rafiki yangu, kazana kila siku kuwa bora, kazana kila siku kupiga hatua mpya, kazana kila siku kujaribu vitu ambavyo hujazoea kufanya.

SOMA; #UKURASA WA 1031; Jinsi Ya Kuwa Sumaku Ya Fedha….

Ndiyo kwenye kujaribu kuna hatari ya kushindwa, lakini pia utajifunza na kuweza kuchukua hatua kubwa zaidi, ambazo zitakuletea matokeo bora na ya tofauti.

Pale unapoona unakazana kufanya kitu kwa kawaida, kufanya kile ambacho umezoea kufanya, kwa sababu unaona ndiyo salama, simama na jiulize je unataka kushinda au kushindwa.

Kama unataka kushinda basi acha kufanya kwa ukawaida na angalia kwa namba gani unaweza kuboresha zaidi.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Dr. Makirita Amani,

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog