Kipimo kizuri cha watu ambao hawafanikiwi, watu ambao hawawezi kupiga hatua zaidi kwenye maisha yao ni ujuzi wa mambo.
Watu ambao hawajafanikiwa tayari wanajua kila kitu.
Waoneshe kitabu na waambie hiki ni kitabu kizuri kwako kusoma. Watakuambia labda hawana muda au hakuna jipya wanaweza kujifunza kwenye kitabu hicho.
Watakuambia waziwazi bila hata ya aibu kwamba mambo yaliyopo kwenye vitabu hivyo ni yale yale.
Hawa ni watu ambao wanaamini wanajua kila kitu, wanajua zaidi kuhusu fedha kuliko hata wale ambao wana fedha zaidi yao. Na hapo ndipo unajiuliza kama kweli wanajua kuhusu fedha, kwa nini hawana fedha hizo?
Ninachotaka kukukumbusha hapa rafiki yangu ni umuhimu wa kujifunza kila wakati na kupitia kila mtu.
Hakuna kitabu chochote ambacho hakuna unachoweza kujifunza, hata kama tayari ulishasoma kitabu hicho, unaweza kusoma tena na ukajifunza mengi ambayo hukuweza kuyang’amua uliposoma kwa mara ya kwanza.
Hakuna mtu yeyote ambaye hana la kukufundisha, kila mtu unayekutana naye kwenye maisha yako, anakuja na kitu cha kukufundisha. Wapo wanaokufundisha ya kufanya, na wapo wanaokufundisha ya kutokufanya.
Kama unajiona unajua kila kitu, jua tu ya kwamba hakuna unachojua na unajizuia sana kufanikiwa.
Huwezi kufanikiwa kama unafikiri unajua kila kitu, na huwezi kuwa bora zaidi kama unafikiri wewe ni zaidi ya wengine.
Kila mmoja wetu ana kitu cha kujifunza, tuwe tayari kujifunza mara zote.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,