Watu wanaotafuta ‘kiki’ ili wawe kwenye maneno ya watu, wanatumia njia sahihi ya masoko, lakini kwa namna ambayo ni mbaya.
Jukumu kuu la masoko ni kuwafanya watu wazungumzie biashara yako au huduma unayotoa. Pale watu wanapokuzungumzia, ndiyo wengi zaidi wanakujua na wao wanatamani kuja kupata huduma ambayo wengine wamepata na wanaizungumzia.
Sasa watu wanaweza kukuzungumzia kwa sifa mbaya, na hilo ni rahisi, kila mtu anaweza kulifanya. Kufanya kitu cha kushangaza, ambacho watu hawakutegemea mtu kama wewe ufanye, hivyo wanakuzungumzia na hilo linawafanya wengi zaidi kutaka kukujua. Hii ni njia rahisi, ambapo pia ina madhara makubwa kwa baadaye, maana watu wanakosa imani juu yako.
Njia nyingine ya watu kukuzungumzia ni kufanya kitu cha thamani sana, ambacho hawakutegemea kabisa kupata, kitu ambacho kinayafanya maisha yao kuwa bora na hawawezi kukipata chochote. Njia hii ni ngumu, inahitaji uweke kazi sana, inahitaji muda na inakwenda kidogo kidogo. Lakini ni njia nzuri, inayodumu na inayowafanya wateja wakuamini na kukutegemea.
Hivyo tengeneza mfumo wako wa masoko uwe ni wa kutoa thamani kubwa sana kwa wateja wako, kiasi kwamba hawawezi kutulia bali watamweleza kila mtu kuhusu thamani waliyopata kwako. Na hiyo ndiyo ‘kiki’ sahihi kwa biashara yako.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,