“Take a good hard look at people’s ruling principle, especially of the wise, what they run away from and what they seek out.”
—MARCUS AURELIUS, MEDITATIONS, 4.38
Tunapaswa kushukuru sana kwa nafasi hii nyingine ya kipekee tuliyoipata leo.
Tumeiona siku hii siyo kwa nguvu au ujanja wetu, bali kwa bahati tu.
Ili kulipa bahati hiyo, tunapaswa kuitendea haki siku hii ya leo, kwa kwenda kuweka juhudi kubwa ili tuweze kupata matokeo bora sana.
Kwa msingi wetu wa NIDHAMU, UADILIFU NA KUJITUMA pamoja na mwongozo wa AFYA, UTAJIRI NA HEKIMA tunakwenda kufanya makubwa leo na kila siku ya maisha yetu.
Asubuhi ya leo tutafakari WAANGALIE WENYE HEKIMA…
Katika kujifunza namna ya kuyaendesha maisha yetu kwa mafanikio, tunapaswa kuwaangalia wale waliofanikiwa jinsi wanavyoendesha maisha yao na kujifunza kwao. Kuangalia nini wanafanya na sisi tufanye na nini hawafanyi na sisi tusifanye.
Katika kujifunza namna ya kuyaendesha maisha yetu kwa haki, tunapaswa kuwaangalia wale wenye haki jinsi wanavyo au walivyoendesha maisha yao. Kujua yapi walifanya na sisi tufanye na yapi hawakufanya na sisi tusifanye.
Chagua watu wenye hekima ambao utajifunza kutoka kwao, wale ambao wamefika pale ambapo wewe unataka kufika.
Kwenye kila eneo la maisha yako, mchague mtu mwenye hekima ambaye utajifunza kwake na pia utajipima kupitia yeye.
Hii ndiyo njia pekee ya mkato na ya uhakika ya kuweza kupiga hatua nzuri kwenye maisha yako.
Njia bora ya kujifunza na kujipima kupitia wengine ni kujiuliza swali ANGEFANYA NINI?
Unaangalia hali uliyopo nayo wewe na kisha kujiuliza kama yule mwenye hekima unayejifunza kwake, angekutana na hali kama yako, je angefanya nini?
Kwa njia hii utaona namna bora ya kufanya kwenye kila hali unayokuwa nayo kwenye maisha yako.
Nikutakie siku bora sana ya leo, siku ya kujifunza na kujipima kupitia wale wenye hekima zaidi kuliko wewe.
#JifunzeKwaWenyeHekima, #JeFulaniAngefanyaNini, #WanachowezaWengineUnawezaPia
Wako rafiki katika safari ya kuelekea mafanikio makubwa,
Kocha Dr Makirita Amani,
http://www.amkamtanzania.com/kocha