Inapokuja kwenye mawazo ya kuanza biashara au ujasiriamali, watu hukabili hilo kwa mitazamo miwili, ambayo inaendana na ufunguo na kufuli.
Wapo ambao wanaanza kutengeneza ufunguo, kisha wanazunguka kutafuta kufuli ambalo litakubali kufunguliwa na ufunguo huo. Hili ni zoezi gumu sana, kwa sababu hata ufunguo uwe mzuri kiasi gani, itakuchukua muda na nguvu kubwa sana kupata kufuli linalokubali kufunguka kwa ufunguo uliotengeneza.
Na wapo wanaotafuta kwanza kufuli ambalo halina ufunguo, kisha wanaweka juhudi kubwa kwenye kutengeneza ufunguo unaoweza kufungua kufuli hilo. Hawa wanapofanikiwa kutengeneza ufunguo, kazi yao kubwa inakuwa imeisha, hawahitaji tena kuzunguka kutafuta kufuli la kufungua, maana tayari lipo.
Kwa upande wa biashara na ujasiriamali, wanaotengeneza ufunguo kwanza kisha kutafuta kufuli ni wale ambao wanatengeneza suluhisho la tatizo kwanza, kisha wanaanza kutafuta nani mwenye tatizo hilo ili wamuuzie suluhisho hilo. Linaweza kuwa suluhisho bora sana, lakini kama inabidi uanze tena kuwatafuta wenye suluhisho, kazi inakuwa ngumu zaidi kwako.
Wanaotafuta kufuli kisha wanatengeneza ufunguo ni wale wanaoangalia matatizo ambayo tayari watu wanayo, kisha kuyatengenezea suluhisho na hapo wanakuwa tayari wana wateja wa uhakika. Hawahitaji tena kwenda kutafuta wateja wala kuwashawishi, tayari wateja wapo na wana tatizo, wanachohitaji ni suluhisho.
Mara zote kaa upande wa kutafuta kufuli kwanza kisha kutengeneza ufunguo, angalia kwanza matatizo ambayo watu tayari wanayo, tengeneza suluhisho na kisha wauzie watu suluhisho hilo. Kazi itakuwa rahisi kwako na utaweza kupiga hatua kubwa.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,