Ushauri wa zamani kwenye mafanikio ulikuwa ni uyajue madhaifu yako, kisha ukazane kuwa imara kwenye madhaifu hayo.
Lakini kitu kimoja kilitokea kwa wale waliofuata ushauri huo, madhaifu yao yalizidi kuwa imara, na yale ambayo walikuwa imara wakawa dhaifu. Hivyo wakaishia kuwa vibaya kuliko walivyokuwa awali.
Ushauri wa sasa kwenye mafanikio ni kujua maeneo ambayo una uimara na kukazana kuwa imara zaidi maeneo hayo, na yale maeneo ambayo una udhaifu kutokujisumbua nayo.
Kwa kufuata ushauri huu, unakuwa imara sana kwenye maeneo machache, na mengine unakuwa dhaifu. Lakini uimara wako kwenye maeneo hayo machache, unafunika ule udhaifu ulionao kwenye maeneo mengine.
Na hapa ndipo udhaifu wako unapokuwa na manufaa kwako, unapochangia kwenye uimara wako, kwa kuutambua na kutohangaika na udhaifu ulionao.
Turudi kwenye mifano ili kuelewa hili vizuri.
Mainjinia wanao uwezo wa kutengeneza gari ambalo ni imara na lenye viwango sana kiasi kwamba hata lipate ajali ya aina gani, waliopo ndani ya gari hilo hawawezi kuumia kabisa.
Lakini sasa, kwa uimara huo wa gari, litakuwa zito sana kiasi kwamba halitaweza kuwa na mwendo wowote na pia litakuwa pana sana kiasi kwamba haliwezi kuenea barabarani.
Kwa hiyo tuko tayari kuyaweka maisha yetu hatarini, ili tuweze kupata mwendo wa kutoka eneo moja na kwenda eneo jingine.
Hivi pia ndivyo unavyopaswa kuyachukulia maisha yako, kuna baadhi ya manufaa unapaswa kuwa tayari kuyaacha yaende kwenye madhaifu uliyonayo na kupeleka nguvu zako kwenye uimara ulionao.
Ukishaujua udhaifu wako na kutokuuruhusu ukusumbue unageuka kuwa uimara kwako.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,
Ni bonge la ukurasa. Kurasa hizi zina mafundisho mazito. Ukiyafuata yanakuepushia mambo mengi sana. Kuna wana kisima cha maarifa wengi hawaingii ndani kabisa ya kisima cha maarifa. Hivyo hujikosesha maarifa muhimu sana. Ndani ya kisima kuna majibu ya maswali mengi sana. Cocha wahamasishe waingie waone uhondo
LikeLike
Asante sana Kasanda,
Ni kweli kabisa, kurasa hizi za kila siku, zina majibu mazito ya kila aina ya changamoto ambayo mtu anaweza kuwa anaipitia kwenye maisha yake,
Na kwa sasa naweka nguvu kubwa sana kwenye kuandaa kurasa hizi, kuzifanya ziwe fupi lakini zenye ujumbe mzito na udumuo.
Ni kweli pia wanachama wengi wa KISIMA hawaingii kuzisoma, na tuna wajibu wa kuwahamasisha wengi kuingia kusoma.
Tusaidiane kwa wale wote ambao huwa mnaingia na kusoma kila siku, kushare kwenye group pia kile ambacho mmejifunza na kuwaalika wengine kuingia kwenye kurasa hizi pia.
Asante sana na karibu tuendelee kuwa pamoja.
LikeLike
Asante kocha kwa ujumbe huu mzuri kwetu. Kujua uimara wangu ni upi na kukazana kuutumia vyema.kuziba pale nilipo na udhaifu.
LikeLike
Karibu Tumaini,
Kweli, tusipoteze nguvu kwenye udhaifu.
LikeLike