Hakuna jambo lolote ambalo una uhakika nalo kwa asilimia 100 kwenye maisha yako. Lolote linaweza kutokea, na mara nyingi mambo ambayo huwa hatutegemei yatokee, huwa yanatokea kwa wakati ambao hatukutegemea yatokee.
Huna uhakika kama kesho utakuwa hai, lakini je hilo linapaswa kukufanya upoteze siku ya leo?
Huna uhakika kama wateja unaowatangazia waje kwenye biashara yako watakuja, lakini je hilo litakuzuia kuitangaza biashara yako?
Huna uhakika kama kazi uliyonayo leo utaendelea kuwa nayo siku zijazo, lakini je hilo litakufanya uifanye kazi hiyo hovyo?
Japokuwa hatuna uhakika na mambo mengi, kuna kitu kimoja tunapaswa kufanya kwenye kila hali ya kutokuwa na uhakika tunayokuwa nayo. Kitu hicho ni kufanya kilicho sahihi.
Kila unapojikuta njia panda, ukiwa hujui ufanye nini, jiulize kipi kilicho sahihi katika hali hiyo na fanya hicho. Fanya kile ambacho ungefanya kama ungekuwa na uhakika na fanya kama vile una uhakika kabisa.
Huna uhakika kama utakuwa hai kesho, lakini ishi leo kama vile una uhakika wa kuwa hai milele. Hilo litakufanya uchukue hatua zilizo sahihi, na kama kesho utakuwepo basi itakuwa bora, hata kama hutakuwepo hiyo kesho, bado utakuwa umeishi vizuri leo.
Kwenye kazi, biashara, mahusiano, fedha na kila eneo la maisha yako, pale unapojikuta njia panda, pale unapojikuta una hali ya kutokuwa na uhakika, fanya kilicho sahihi, fanya kama vile una uhakika wa asilimia 100.
Kwa kufanya hivyo haimaanishi kwamba hutakosea, kuna makosa utayafanya, lakini itakuwa bora kuliko kutokufanya chochote kabisa. Hatua yoyote utakayochukua ni bora kuliko kutokuchukua hatua kabisa.
Usikubali tena kukwama kwenye jambo lolote kwa sababu huna uhakika, jiulize kipi sahihi kufanya, jiulize kama ungekuwa na uhakika ungefanya nini, kisha anza kufanya hicho kwa uhakika.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,