“It never ceases to amaze me: We all love ourselves more than other people, but care more about their opinion than our own.” — Marcus Aurelius
Kila mtu huwa anajipenda mwenyewe kuliko anavyowapenda wengine.
Hii ndiyo njia pekee iliyotuwezesha sisi binadamu kufanikiwa.
Maana kwa kujipenda na kujijali, inakuwa rahisi kuwapenda na kuwajali wengine pia.
Lakini kuna jambo moja la kushangaza, licha ya kujipenda wenyewe, huwa tunajali sana maoni ya wengine kuliko maoni yetu binafsi.
Tunaweza kupanga kufanya kitu fulani na kuamini tunaweza kukifanya lakini tunapowaambia wengine kuhusu hilo na wakatuambia hatuwezi au haiwezekani tunawasikiliza na kuwaamini.
Tunafikiri kila maoni anayotoa mtu mwingine ni ukweli, na hapo ndipo tunapokwama.
Asubuhi ya leo tafakari ni mambo mangapi umeacha kuyafanya kwenye maisha yako kwa sababu ya maoni ya watu wengine.
Fikiria mambo yote ambayo ulikuwa na hamasa kubwa ya kuyaanzisha, lakini baada ya kukatishwa tamaa na wengine umeyaacha.
Kama usingesikiliza maoni ya wengine, ungekuwa umepiga hatua kubwa.
Kuanzia sasa thamini maoni yako kuliko ya watu wengine.
Kama kuna kitu umepanga au unataka na unaamini hicho ndiyo sahihi kwako basi fanya kama ulivyopanga na usijali maoni ya wengine yanasemaje.
Kila mtu ana haki ya kuwa na maoni yake kwenye jambo lolote, lakini hulazimishwi kufuata maoni ya yeyote yule.
Yape maoni yako kipaumbele na kamwe usiache kufanya chochote kwa sababu ya maoni ya wengine.
#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
Ukurasa wa leo ni kuhusu tabia kupiga kelele kuliko maneno, soma zaidi hapa; http://www.kisimachamaarifa.co.tz/2020/10/24/2124
Rafiki yako,
Kocha Dr Makirita Amani.