2317; Kukimbiza Kipepeo…
Kutafuta furaha kwenye maisha ni sawa na kumkimbiza kipepeo. Kadiri unavyomkaribia ndivyo anavyozidi kukimbia zaidi.
Lakini usipomkimbilia kipepeo, ukiwa ‘bize’ na mambo yako mengine, unashangaa kipepeo anakufuata mwenyewe.
Ukifanya kitu kwa sababu unategemea kupata furaha unaishia kutokuipata furaha, hata kama umekikamilisha inavyopaswa.
Lakini unapokuwa ‘bize’ kufanya kitu kwa sababu umechagua kukifanya na umeamua kukifanya kwa ubora wa hali ya juu sana, unajikuta ukiwa na furaha kubwa katika kufanya kitu hicho.
Hivyo njia ya uhakika ya kuwa na maisha ya furaha ni kuacha kabisa kuizungumzia furaha na kujisalimisha kwenye wajibu mkubwa kuliko ulivyozoea.
Katika kutimiza wajibu huo, unapata furaha japo hilo siyo lengo.
Ukishaifanya furaha kuwa lengo, hapo hapo unakuwa umeipoteza, maana hata unapofikia lengo ulilojiwekea, utaona jingine kubwa zaidi na kila wakati utakuwa unaiahirisha furaha.
Fanya furaha kwako kuwa ni matokeo na siyo lengo. Sahau kabisa kitu kinachoitwa furaha na wewe kuwa bize kuyaishi maisha yako na kutimiza kusudi lako.
Ukiikimbiza furaha itakukimbia maisha yako yote, ukiachana nayo na kupambana na makubwa itakufuata kila wakati.
Kocha.