2454; Ukitaka sana kitu, unakifukuza.

Pale unapokuwa unakitaka sana kitu na kutaka kukipata kwa wakati unaotaka wewe mwenyewe, huwa inakuwa vigumu zaidi kukipata.

Utakazana na kulazimisha sana ukipate, utatumia kila aina ya njia.
Lakini kadiri unavyohangaika ili kukipata, ndivyo kinakwenda mbali na wewe.

Cha kushangaza sasa, pale unapokuwa hakitaki sana kitu, pale unapokuwa huangalii sana nini unataka kupata, ndiyo inakuwa rahisi sana kwako kupata.
Yaani unashangaa vitu vinakuja kwako kwa urahisi sana, bila hata ya kutumia nguvu kubwa.

Ni kanuni ya asili kwamba pale unapokitaka sana kitu kinakukimbia.
Pale unapowalazimisha sana watu wakupe au wafanye kitu fulani ndiyo wanakataa kabisa.

Njia ya kutatua hili ni kuweka tamaa na matakwa yako pembeni na kuangalia kile wengine wanataka kisha wapatie.
Unapokuwa umetingwa kufanya vitu kwa ajili ya wengine, unashangaa mahitaji yako nayo yanatimia bila hata ya kuweka nguvu kubwa kwenye hilo.

Hili lipo hata kwenye mawazo, kama kuna kitu unajilazimisha sana kukikumbuka kwa haraka, inakuwa vigumu sana kukikumbuka.
Lakini ukiachana nacho na kufikiria mambo mengine, unashangaa kumbukumbu zinakuna zenyewe.

Usilazimishe sana kile unachotaka kwa wakati unaotaka, peleka nguvu zako kwenye mambo mengine na unachotaka kitakuja kwako chenyewe.

Hatua ya kuchukua;
Fikiria kitu ambacho umekuwa unakitaka sana na kuhangaika nacho muda wote na jinsi kimezidi kuwa kigumu kwako kupata.
Amua sasa kuacha kukifikiria na kukitaka sana na peleka juhudi zako zote kwenye kile unachofanya au kutoa kwa ajili ya wengine.
Hakikisha unatoa thamani kubwa sana kwa ajili ya wengine kwenye kile unachofanya.
Na siku usiyotegemea, utashangaa kile ulichokuwa unataka kinakuja kwako, bila hata ya kuweka nguvu kubwa kwenye kitu hicho.

Tafakari;
Jisahau wewe mwenyewe katika kuwahudumia wengine. Yaani wewe angalia wengine wanataka nini na uwapatie, badala ya kuangalia unataka nini ili upate zaidi.
Kwa kukazana kuwahudumia wengine na kuyasahau matakwa yako kwa muda, utapata kila unachotaka kwa wakati wake.
Kilicho ndani ya uwezo wako nj juhudi unazoweka na siyo matokeo unayopata. Hangaika na juhudi na siyo matokeo na hutaumia pale mambo yanapokwenda tofauti na matakwa yako.

Kocha.