3129; Ni kodi unayotakiwa kulipa.

Rafiki yangu mpendwa,
Maisha yetu yamekuwa magumu na yenye changamoto mbalimbali kwa sababu ya matarajio yasiyokuwa sahihi ambayo tunakuwa nayo.

Tunataka dunia iende kama tunavyotaka sisi wenyewe, wakati dunia haijui hata kama tupo hai.
Dunia huwa inajiendesha kwa kanuni zake za asili, bila ya kujali nini sisi tunataka au hatutaki.

Kwa mfano kama unataka kufanya kazi zaidi, lakini giza limeingia, unaweza kuvurugwa utakavyo, lakini huna cha kufanya.
Dunia haiwezi ghafla ikaanza kukuangalia wewe ni muda wa mwanga kiasi gani unahitaji ili ikupe. Yenyewe itaendelea kujizungusha kwenye mhimili wake na kuleta usiku na mchana kwa usawa.

Maisha tunayoishi hapa duniani, yana kodi mbalimbali ambazo tunapaswa kuzilipa.
Kujaribu kukwepa kodi hizo ndiko kumekuwa chanzo kikubwa cha changamoto kwa maisha ya wengi.

Hapa sizungumzii kodi ambazo unajua kabisa unatakiwa kulipa, kama vile za nyumba au za serikali.
Bali nazungumzia gharama mbalimbali za aina ya maisha unayochagua kuishi hapa duniani.

Kuoa au kuolewa kunakuja na manufaa yake, lakini pia kunaambatana na gharama za kulipa. Kadhalika kutokuoa au kuolewa, kunakuwa na gharama zake za kulipa.

Kuajiriwa kuna manufaa yake fulani, lakini pia kunaambatana na gharama za kulipa.
Kadhalika kufanya biashara, kuna manufaa na gharama.
Ni uchague kipato kidogo na cha uhakika au kipato kikubwa kisichokuwa cha uhakika.

Kushirikiana na watu wengine kwenye jambo lolote lile kuna manufaa ya kupata mchango wa wengine.
Lakini pia kunakuja na gharama ya kuchelewa kufanya maamuzi kwa sababu wengine lazima pia wahusishwe.
Na hapo bado kuna hali za kutokuelewana baina ya watu.

Kutokufanikiwa kuna gharama ya kudharauliwa na kupuuzwa na wengine. Wakati kufanikiwa kuna gharama ya kuchukiwa na kuwindwa na wengine.
Kabla hujafanikiwa unaweza kuona maisha ni magumu sana kwako na kudhani kwa kufanikiwa utayarahisisha.
Utapambana sana ili ufanikiwe, halafu ndiyo unagundua mafanikio nayo yanakuja na gharama zake pia.

Huwa nacheka sana pale mtu anaponiambia lengo lake ni kumaliza kabisa changamoto anazopitia kwenye maisha.
Najiambia huyu hajui anachopanga, utatuzi wa changamoto moja ni uzao wa changamoto nyingine.
Ndivyo maisha yanavyokwenda, huwezi kukwepa hilo.

Hivyo basi, badala ya kukwepa kila aina ya changamoto, ni vyema kujiandaa kuzikabili changamoto kubwa zaidi.
Badala ya kuangalia maisha yasiyokuwa na gharama, ni vyema kujiandaa kulipa gharama kubwa zaidi.

Kila maisha yanapoleta changamoto kwako, usichukie wala kulalamika, badala yake furahia, kwa sababu ni ishara kwamba unakua.
Kama changamoto ulizonazo ni zile zile ambazo umekuwa nazo mara zote, haimaanishi kwamba wewe ni mjanja sana, bali inamaanisha unabaki pale pale, hukui.

Kwa mfano, unapoanzisha biashara yako, ambayo unakuwa peke yako, unakuwa na udhibiti mkubwa wa biashara hiyo. Lakini unakuwa na changamoto kubwa sana za uchovu wa kufanya kila kitu peke yako na huo unakuzuia kukua.
Unapoamua kuajiri wafanyakazi kwenye biashara hiyo ili utatue changamoto yako ya uchovu, utaitatua, lakini utakuwa umezalisha changamoto nyingine mpya, ambayo ni ya usimamizi wa watu.
Watu wana tabia zao mbalimbali ambazo ni tofauti kabisa na za kwako.
Ungetamani wakupe tu kazi unayotaka na waweke tabia zao pembeni, lakini kwa bahati mbaya wanaambatana na hizo tabia, kama boga na ua lake.
Hivyo unakuja kukuta tabia binafsi za wafanyakazi wako kwenye biashara, zinaiathiri biashara pia.
Na hapo unakuwa na gharama za ziada za kusimamia tabia hizo binafsi zisiathiri biashara unayojenga.

Hivyo ndivyo maisha yanavyokwenda hapa duniani.
Hakuna kitu cha bure.
Huidai dunia chochote.
Inakupa hifadhi.
Kuna gharama lazima uzilipe.
Unaweza kuchagua kuzilipa na kukua zaidi.
Au ukazilalamikia na ukabaki pale ulipo.
Maisha ni yako na uchaguzi ni wako.
Malalamiko yoyote unayoweza kuwa nayo, hayamwathiri mtu mwingine yeyote isipokuwa wewe.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe