3224; Wakikuonyesha usiwakatalie.

Rafiki yangu mpendwa,
Tunawahitaji sana watu kwenye maisha yetu.
Na kadiri tunavyokuwa tunawahitaji watu fulani, ndivyo tunavyotamani wangekuwa vile tunavyotaka wawe.

Mwanzoni watu huwa wanaweza kudanganya na kuigiza vile tunavyotaka.
Na huwa tunahadaika na hilo.
Na kufurahi kwa sababu tunaona tumewapata watu sahihi.

Lakini uongo na maigizo huwa hayadumu kwa muda mrefu.
Huwa haichukui muda watu hao huwa wanaanza kutuonyesha uhalisia wao.
Wanaanza kuwa wao, ambao ni tofauti na tulivyotegemea.

Unaweza kudhani baada ya watu kutuonyesha uhalisia wao, tungekubali na kuachana nao pale uhalisia huo unapokuwa tofauti na mategemeo yetu.
Lakini cha kushangaza huwa tunawakatalia.
Tunaona wameteleza tu.
Na kusubiri kwamba watabadilika.

Lakini uhalisia wa watu ndiyo ngozi yao halisi.
Huwa hawabadiliki, bali wanaendelea kuwa hivyo.
Lakini bado tunakuwa na matumaini ya wao kubadilika na kuwa kama vile tunavyotaka sisi.
Wanaweza hata wakaahidi kubadilika.
Lakini bado uhalisia wao utakuwa na nguvu, wanajikuta wanarudi kwenye uhalisia huo.

Rafiki, usitamani watu wawe tofauti, bali tamani wajidhihirishe mapema.
Usitamani watu wawe vile unavyotaka wewe, bali tamani kuujua uhalisia wao.
Na pale watu wanapokuonyesha uhalisia wao, usiwakatalie kwa kutaka wawe tofauti.
Wala usiumie kwa sababu ulitaka wawe tofauti.

Unachopaswa ni kupima, kwa uhalisia ambao umeujua kuhusu watu, je bado mnaweza kwenda pamoja na kila mtu akanufaika?
Kama jibu ni ndiyo basi nendeni pamoja na kila mtu anufaike.
Lakini kama jibu ni hapana basi kila mtu aende na njia yake.

Hapo kwa kila mtu kwenda njia yake ndiyo huwa pagumu zaidi.
Kwa sababu tunaona kama hatuwezi kupata watu wengine sahihi.
Lakini huo siyo ukweli, watu ni wengi na kati yao watakuwepo wale ambao uhalisia wao ndiyo tunauhitaji.
Tunachohitaji ni kuweka kazi mpaka kuwafikia watu hao sahihi.

Kila wakati tunapaswa kuwa kwenye msako wa kutafuta watu wa kushirikiana nao kwenye maeneo mbalimbali ya maisha yetu.
Hii ni kuanzia wateja kwenye biashara zetu, wafanyakazi, washirika, marafiki, watu wa kuambatana nao n.k.
Zoezi la kutafuta watu hao halipaswi kukoma, kwa sababu watu unaoanza nao siyo wote utakaoenda nao kwa muda mrefu.
Kadiri muda unavyokwenda utagundua kuna ambao huwezi kwenda nao zaidi.
Siyo kwa sababu ni watu wabaya au hawafai, ila ni kwa sababu uhalisia wao hauendani na kile unachotaka kwao.

Hii dunia tayari inao watu wengine,
Na wengine wapya wanazaliwa na kukua kila siku.
Katika hao wengi, wapo ambao uhalisia wao unaendana na kile unachotaka wewe.
Inahitaji wewe uweke kazi kubwa kuwafikia hao halisi.
Ukiacha uvivu na kuweka kazi, utawafikia hao sahihi na kuacha kuwalaumu wale ambao uhalisia wao umekuwa tofauti na mategemeo yako.

Mwisho kabisa, usipuuze viashiria ambavyo watu wanavionyesha mapema kabla ya kujidhihirisha ni watu wa aina gani.
Kwa sababu watu huwa wanatoa viashiria vingi vya namna walivyo.
Ila kwa kuwa tunakuwa tunawahitaji sana, tunapuuza viashiria hivyo, kwa kuona labda walipitiwa.
Tunaenda hivyo mpaka pale tunapopata madhara makubwa ndiyo tunaona ndivyo watu walivyo.
Na hata baada ya kupata madhara hayo, bado hatukubali, tunaona watu hao watabadilika, hivyo tunaendelea kudhurika zaidi na zaidi.

Tujikumbushe hili mara zote; watu wakituonyesha uhalisia wao, tusiwakatalie, tujue ndivyo walivyo na mabadiliko huwa hayatokei kwa sababu ndiyo kitu tunachotaka.
Watu wapo wengi, tukazane kutafuta wale ambao uhalisia wao unaendana na vile tunavyotaka sisi na kazi yetu itakuwa rahisi kuliko kutaka watu wabadili uhalisia wao na kuwa vile tunavyotaka.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe